Ticker

6/recent/ticker-posts

Elimu Jumuishi Iwe Daraja La Fursa Sawa Kwa Watu Wenye Ulemavu

 


Na Ahmed Abdulla

Elimu ni haki ya msingi kwa kila mwanadamu, bila kujali hali yake ya kimwili, kiakili au kihisia.

Kwa kutambua umuhimu wa haki hiyo, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kushirikiana na wadau mbalimbali, wakiwemo Idara ya Maendeleo ya Jamii ya Kanisa Katoliki Jimbo la Zanzibar kupitia Mradi wa Uwezeshaji wa Jamii kwa Ajili ya Haki za Binadamu na Utawala Bora unaotekelezwa na idara hiyo, wanaendelea kuhamasisha elimu jumuishi ili kuhakikisha watoto wenye ulemavu wanapata fursa sawa za kujifunza, na kushiriki kikamilifu katika Shughuli za kielimu.

Kwa watu wenye ulemavu, elimu jumuishi si huduma ya ziada bali ni haki ya msingi inayowawezesha kupata maarifa, kujitegemea na kushiriki kikamilifu katika maisha ya kijamii na kiuchumi. Watoto na watu wenye ulemavu wanapopewa nafasi ya kujifunza pamoja na wenzao katika mazingira salama na rafiki, hujengewa kujiamini, huondolewa vikwazo vya ubaguzi na kupewa nafasi ya kufikia ndoto zao.

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Sheria ya Watu Wenye Ulemavu ya Zanzibar Na. 8 ya mwaka 2022, inayotambua haki ya kupata elimu, kushiriki katika shughuli za maendeleo na kupata huduma mbalimbali bila ubaguzi imeendelea kuweka mazingira mazuri ya kulinda haki za watu wenye ulemavu.

Sambamba na juhudi hizo, taasisi zisizo za kiserikali na mashirika ya dini zimeendelea kushirikiana na serikali katika kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa kuwajumuisha watu wenye ulemavu katika nyanja zote za maisha.

Aidha, sera mbalimbali za maendeleo ya jamii na elimu zinasisitiza usawa wa fursa kwa wananchi wote ili kuhakikisha hakuna anayebaki nyuma katika safari ya maendeleo ya Zanzibar.

"Elimu jumuishi si msaada kwa watu wenye ulemavu, bali ni haki yao ya msingi na msingi wa kujenga jamii yenye usawa."

Akizungumza na makala hii, Katibu wa Baraza la Watu Wenye Ulemavu Zanzibar, Ussi Khamis Debe, alisema elimu jumuishi ni nyenzo muhimu ya kuwapa watu wenye ulemavu uwezo wa kujitegemea na kushiriki kikamilifu katika shughuli za kijamii na kiuchumi.

Alisema ili kufanikisha azma hiyo, ni muhimu shule zote kuwa na miundombinu rafiki kwa watu wenye ulemavu, walimu wenye ujuzi wa elimu maalumu pamoja na vifaa vya kufundishia vinavyokidhi mahitaji ya wanafunzi wote.

"Jamii inapaswa kuacha tabia ya kuwaficha watoto wenye ulemavu majumbani. Watoto hao wanapaswa kuandikishwa shule mapema kama watoto wengine ili wapate haki yao ya msingi ya elimu na kujenga maisha yao ya baadaye," alisema.

Aliongeza kuwa elimu ndiyo njia bora ya kupunguza utegemezi kwa watu wenye ulemavu na kuongeza idadi ya wananchi wenye uwezo wa kuchangia maendeleo ya taifa.

Kwa upande wake, Awena Hassan Ali, kijana mwenye ulemavu wa kuona ambaye pia ni mwalimu wa Skuli ya Msingi Kisiwanduwi na mkazi wa Shehia ya Kitope, alisema elimu ndiyo iliyompa ujasiri wa kujiamini, kujitambua na kushiriki kikamilifu katika jamii.

Alisema safari yake ya kutafuta elimu haikuwa rahisi kutokana na changamoto mbalimbali alizokutana nazo, lakini hakukata tamaa kwa kuwa aliamini elimu ndiyo njia ya kutimiza ndoto zake.

"Nilikutana na mitazamo hasi kutoka kwa baadhi ya watu waliodhani siwezi kufanikiwa kutokana na ulemavu wangu. Lakini leo hii mimi ni mwalimu na ninaendelea kulitumikia taifa kama wananchi wengine," alisema.

Awena alitoa wito kwa vijana wenye ulemavu kutumia kila fursa ya elimu inayopatikana, huku akizitaka taasisi za elimu kuendelea kuboresha mazingira ili yawe rafiki kwa wanafunzi wote bila kujali hali zao.

Baadhi ya wazazi waliozungumza na makala hii, akiwemo Naima Hamad na Omar Fakih, walisema watoto wenye ulemavu wana uwezo sawa wa kujifunza endapo watapatiwa mazingira yanayowawezesha kuonyesha vipaji na uwezo wao.

Walisema wazazi wana wajibu mkubwa wa kuwahamasisha watoto wao kwenda shule na kushirikiana na walimu katika kufuatilia maendeleo yao ya kitaaluma.

Aidha, walisisitiza kuwa kuwaficha watoto wenye ulemavu majumbani ni kuwanyima haki yao ya elimu na nafasi ya kutimiza ndoto zao, wakieleza kuwa ushirikiano kati ya familia, shule na jamii ndiyo msingi wa mafanikio ya watoto hao.

Elimu jumuishi ni msingi wa kujenga jamii yenye usawa, haki na maendeleo endelevu. Kila mtoto, bila kujali aina ya ulemavu alionao, anastahili kupata fursa sawa ya elimu bora itakayomwezesha kutimiza ndoto zake na kuchangia maendeleo ya taifa.

Pamoja na juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Sheria ya Watu Wenye Ulemavu ya Zanzibar Na. 8 ya mwaka 2022, mchango wa wadau mbalimbali unaendelea kuwa nguzo muhimu katika kuimarisha elimu jumuishi.

Miongoni mwa wadau hao ni Idara ya Maendeleo ya Jamii ya Kanisa Katoliki Jimbo la Zanzibar, ambayo kupitia Mradi wa Uwezeshaji wa Jamii kwa Ajili ya Haki za Binadamu na Utawala Bora inaendelea kuhamasisha jamii kuhusu haki za watu wenye ulemavu, kupinga ubaguzi na kuhimiza upatikanaji wa elimu kwa wote.

Ni wajibu wa wazazi, viongozi wa dini, walimu, viongozi wa jamii, taasisi za umma na binafsi pamoja na wananchi kwa ujumla kuhakikisha hakuna mtoto anayebaki nyuma kwa sababu ya ulemavu. Jamii inayowapa watu wenye ulemavu fursa sawa za kujifunza na kushiriki katika maendeleo ndiyo jamii inayojenga utu, usawa na mustakabali bora kwa vizazi vya sasa na vijavyo.

 

Post a Comment

0 Comments