Na Ahmed Abdulla:
Utelekezaji wa
watoto ndani ya familia umeendelea kuwa miongoni mwa changamoto zinazozikabili
familia nyingi nchini, huku ukiathiri ustawi wa watoto, wanawake na maendeleo
ya jamii kwa ujumla. Licha ya kuwepo kwa sheria zinazolinda haki za watoto,
bado wapo watoto wanaokosa matunzo, malezi na huduma muhimu kutokana na baadhi
ya wazazi au walezi kushindwa kutekeleza wajibu wao.
Akizungumza na
makala hii, Mratibu wa Mradi wa Uwezeshaji wa Jamii kwa Ajili ya Haki za
Binadamu na Utawala Bora chini ya Idara ya Maendeleo ya Jamii, Kanisa Katoliki
Jimbo la Zanzibar, Sister Editha Asiimwe, amesema utelekezaji wa watoto bado
unaathiri ustawi wa watoto wengi na familia zao, hasa pale wazazi au walezi
wanaposhindwa kutekeleza wajibu wao wa msingi.
Amesema mtoto
anapokosa haki zake za msingi kama chakula, elimu, huduma za afya, malazi na malezi
bora, huathirika kimwili, kiakili na kisaikolojia, hali ambayo huathiri
mustakabali wake na maendeleo ya jamii kwa ujumla.
"Mtoto ni
amana kutoka kwa Mwenyezi Mungu, hivyo kila mzazi ana wajibu wa kuhakikisha
anapata haki zake zote za msingi. Kutotekeleza wajibu huo ni kumnyima mtoto
fursa ya kufikia ndoto zake," amesema Sister Editha.
Ameeleza kuwa
kupitia Mradi wa Uwezeshaji wa Jamii kwa Ajili ya Haki za Binadamu na Utawala
Bora, Idara ya Maendeleo ya Jamii inaendelea kutoa elimu ya sheria kwa
wananchi, kujenga uwezo wa wasaidizi wa sheria, kushirikiana na viongozi wa
shehia pamoja na wadau mbalimbali katika kutatua migogoro ya kifamilia
inayochangia utelekezaji wa watoto.
Kwa mujibu wake,
lengo la mradi huo ni kuhakikisha haki za watoto zinalindwa, wazazi
wanawajibika kutekeleza majukumu yao kwa mujibu wa sheria na jamii inakuwa na
uelewa wa kutosha kuhusu wajibu wa kila mmoja katika malezi ya watoto.
Kwa upande wa
jamii, Asha Ali, mama wa watoto wawili kutoka Kaskazini B Unguja, amesema baada
ya kuachwa na mume wake amebaki akigharamia mahitaji yote ya watoto wake,
ikiwemo chakula, elimu na huduma za afya, jambo linaloongeza ugumu wa maisha.
Naye Mwanahamisi
Juma, mwanafunzi mwenye umri wa miaka 15, amesema migogoro ya wazazi huwaathiri
watoto moja kwa moja kwa kuwanyima utulivu wa kisaikolojia na wakati mwingine
kuwafanya washindwe kuendelea vizuri na masomo kutokana na kukosa mahitaji muhimu.
Mzazi Salum Hassan
amesema jamii inapaswa kuendelea kuelimishwa kuhusu wajibu wa wazazi kwa
watoto.
"Kila mzazi
anatakiwa kutambua kuwa malezi ya mtoto ni jukumu la wazazi wote wawili bila
kujali tofauti zao. Watoto hawapaswi kuathiriwa na migogoro ya wazazi,"
amesema.
Mratibu wa Wanawake
na Watoto wa Shehia ya Kitope, Sheni Mohd Juma, amesema ofisi yao hupokea na
kushughulikia migogoro ya kifamilia pamoja na kufuatilia kesi zinazohusu
watoto, huku akisisitiza umuhimu wa ushirikiano wa jamii katika kulinda haki za
watoto.
Kwa upande wa
viongozi wa dini, Sheikh Salum Gharib Salum amesema dini zinawataka wazazi
kuwalea na kuwahudumia watoto wao, huku akieleza kuwa mzazi anayeshindwa
kutekeleza wajibu wake anakiuka mafundisho ya dini.
Naye Mchungaji
Emmanuel Malingila wa Kanisa la Tanzania Assembly of God (TAG) Kitope amesema
wazazi wanapaswa kuhakikisha watoto wanapata malezi bora, elimu, mavazi, malazi
na mahitaji mengine ya msingi ili waweze kufikia ndoto zao.
Aidha, Hamis Juma
Omar, baba wa mtoto mmoja, amesema migogoro ya ndoa mara nyingine huonekana
kuwa ni kosa la upande mmoja, ilhali wakati mwingine pande zote mbili huchangia
changamoto zinazoathiri watoto. Amesisitiza wazazi kutanguliza maslahi ya mtoto
hata pale wanapoamua kuachana.
Msaidizi wa Sheria
wa Shehia ya Kitope, Makungu Hamad Mwinyi, amesema wananchi wengi bado
hawafahamu haki za watoto na taratibu za kuzidai. Amesema wasaidizi wa sheria
wameendelea kutoa elimu ya bure ili kuongeza uelewa wa jamii.
"Kumtelekeza
mtoto si suala la kifamilia pekee, bali ni ukiukwaji wa haki za mtoto unaoweza
kuchukuliwa hatua za kisheria," amesema.
Kwa ujumla, wadau
mbalimbali wanaamini kuwa kupambana na utelekezaji wa watoto kunahitaji
ushirikiano wa wazazi, viongozi wa dini, viongozi wa shehia, wasaidizi wa
sheria, taasisi za serikali na mashirika ya maendeleo. Wanasema kila mtoto
anastahili kuishi katika mazingira salama yenye malezi bora, ulinzi na upendo
ili aweze kukua na kuchangia maendeleo ya taifa.


0 Comments