Ticker

6/recent/ticker-posts

Ni Upi Umuhimu Wa Kwenda Kliniki Mapema Kwa Mama Mjamzito?

 


Na Nihifadhi Abdulla Issa :

Nilikwenda  kijiji cha Kibele, karibu kilomita 30 kusini mwa mji wa Unguja, na kujikuta nafurahia upepo mwanana wa miti iliyokuwepo kila pembe ya kijiji hiki.

Hapo nikakutana na mama mja mzito akifanya  mazoezi mepesi kwa kufanya shughuli za nyumbani huku akijitayarisha kwenda kliniki kuangalia afya yake na kupata ushauri wa wataalamu wa afya ya uzazi.

Mwana mama huyu Mwatum Haji ni kijana wa miaka 35, aliniambi aliona mabadiliko katika mwili wake ambayo yameambatana na uchovu wa mwili na kizunguzungu kilichosababisha kupoteza hamu ya kula na kulala mara kwa mara.

Hali ya mama huyu ilidumu kwa takriban wiki moja bila kuona mabadiliko yoyote jambo lilomshangaza hadi palipotokea mabadiliko ya ya mzunguko wake wa hedhi.

Aliniambia alipata mshituko na kuamua kwenda kituo cha Afya cha Tunguu, kilichopo masafa mafupi na kijiji chake na kukutana na wataalamu wa Afya ambao walimpima mkojo ili kujuwa kama ni mjamzito au anasumbuliwa na maradhi mengine.

Baada ya vipimo aligundulika  ameshika ujauzito wa mwezi mmoja na kushauriwa mambo muhimu yanayohusu afya yake, ikiwa pamoja na kuhudhuria kliniki mapema na kwa wakati.

Tokea wakati huo akawa kiguu na njia kila baada ya muda kufunga safari yake ya kwenda kliniki ambapo alikuwa anapata vipimo na ushauri kwa usalama wa afya yake na kiumbe kilichokuwa tumboni mwake.

Alisema amejifunza umuhmu na faida ya kuhudhuria kituo cha afya mapema kwa mama mja mzito kwani mimba inapokuwa changa matatizo yanakuwa mengi .

“Nimepata somo katika mimba yangu hii ya tatu kwani kwa mimba zilizopita nilichelewa kuhudhuria kliniki mapema.

Matokeo yake nilipata matatizo mbali mbali, ikiwemo kupoteza damu mara kwa mara lakini kwa mimba hii kwa kwenda kliniki  mapema nimepata elimu ilionisaidia kuondokana na matatizo ya mimba ziliopita,” alisema huku akitabasamu.

 

MTAZAMO WA WANAUME KWA WAKE ZAO KUHUDHURIA KLINIKI MAPEMA

Juma Ali (37) (sio jina lake rasmi) wa Tunguu, alisisitiza kwamba upo umuhimu wa mama wajawazito kuhudhuria kliniki mapema kwa sababu kufanya hivyo kuna faida nyingi na kuchelewa kuna athari zake.

 Aliwataka wanawake wasifanye uvivu wa kuchelewa kwenda kliniki na kuwashauri kuwasikiliza wataalamu wa afya.

Juma ambaye amesomea taaluma ya afya ya uzazi alitahadhaisha kwamba mtu ambaye hafuati maelekezo ya madaktari anaweza kupata matatizo ambayo yangeweza kuepukika.

Omar Abdalla (40) mkaazi wa Ndijani, alisema humshauri mke wake kuhudhuria mapema mara tu anapona viashiria vya ujauzito ili kupata elimu ya ziada ya namna nzuri ya kuilea mimba.

“ Mtoto ni neema na baraka kutoka kwa Allah wanikuna watu wanatamani kupata watoto, lakini hawajaaliwa. Nikiona viashiria tu vya ujauzito kwa mke wangu jambo la kwanza namshauri aende kliniki kupata ushauri juu ya afya yake  na namna gani tutashirikiana kulea hiyo mimba,” alieleza Omar Abdalla, Mkaazi wa Ndijani.

Bashir Rajab Mtumweni (32) pia wa Tunguu , alisema umuhimu wa wajawazito kuhudhuria kliniki mapema ni kugunduwa athari za kiafya, kama zipo,  mapema ni kupata kinga na matibabu maema kwa mama na mwanawe aliyembeba tumboni.

 

Alieleza kwamba mke wake wakati akiwa mjamzito alipata matatizo ya fuko lake la uzazi kuwa jepesi, lakini alipohudhuria kliniki mapema alipewa ushauri wa kupunguza kufanya kazi za nguvu na kutumia muda mwingi kupumzika na hii ilimsaidia.

“Baada ya kuarifiwa hali hio nilimpunguzia mke wangu majukumu ya kazi na kuwajibika mwenyewe kwa majukumu ya ndani,  alieleza Bashir Rajab, Mkaazi wa Tunguu.

Katika hii ziara maalum ya  vituo vya afya vyaWilaya ya Kati na Magharibi “B” tulifika kituo cha Afya Mwera na kuwakuta mama wajawazito waliopanga foleni kusubiri  zamu zao za kuonana na daktari.

Hapo Mwera nilizungumza na Samir Salim (40) ambaye alisema anatoa mashirikiano mazuri kwa mkewe anapogundua  ni mjamzito na humsaidia majukumu ya nyumbani, ikiwa pamoja na kuhudumia watoto.

“Majukumu ni ya kwetu sote, lakini mke wangu anapokuwa mjamzito nafanya kazi za nyumbani ili apumzike na kulea ujauzito akiwa na amani.Hii ni kwa sababu na kiumbe kilichopo tumboni nacho kinahitaji kupumzika vyemaili afya yake iimarike’’, alisistiza.

Bi Asha Faki (34), mkaazi wa hapo Mwera ni mama mwenye watoto wawili na alikuwa na uja uzito wa tatu uliokua na miezi mitano. Hii ilikuwa mara yake ya kwanza kuhudhuria kliniki.

Mama huyu alisema hakuwa anahudhuria kliniki mapema pindi kwa kuhofia  aibu ya kusemwa na wanawake wenzake, hivyo husubiri angalau miezi mitano pale tumbo likianza kuchomoza.

Alikiri wakati akivuta muda wa kwenda kliniki alikuwa anakabiliwa na matatizo, ingawa sio makubwa. Haya ni kujiona mchofu, hasa anapoamka asubuhi,  miguu kuvimba na  anakosa hamu ya kula.   

USHAURI WA WATATALAMU WA AFYA

Khatib Ramadhan Haji, Afisa Tabibu na Mkuu wa  kituo cha Afya cha daraja la kwanza cha Tunguu ambacho kinahudumia shehia za Tunguu, Jumbi, Binguni na Bungi , zenye wastani wa wagonjwa 10,000 alisema wanawake wenye matarajio ya kubeba ujauzito ama wenye uwezo wa kujifunguwa  ni 4,200.

“Sisi tunatoa e elimu ya afya ya uzazi na kuhimiza waja wazito kuhudhuria kliniki  mapema ili kuepuka athari zinazoweza , kama vile magonjwa yanayoweza kutibiwa  au kukingwa mapema,”  alieleza Khatib Ramadhan Haji, Afisa Tabibu  wa Kituo cha Afya Tunguu.

Kituo cha Tunguu kinatowa huduma za upimaji wa mama wajawazito,  chanjo zote kwa wasichana na watu wazima, upimaji na lishe kwa watoto na elimu ya afya ya uzazi ambayo inajumuisha chakula kinachowajenga kiafya mama wajawazito.

Afisa Muelimishaji na Muhamasishaji wa Afya ya Uzazi, Mama na Mtoto katika Wizara ya Afya Zanzibar, Kitengo Shirikishi cha Mama na Mtoto, Fatma Ussi Yahya, alisema kitengo  kinatowa elimu kupitia vyombo vya habari ili  kuelimisha jamii kujuwa afya zao mapema kwa sababu kipindi cha mwanzo cha ujauzito huwa na mabadiliko ya mwili.

Alisema wanelimisha akina baba wanapogunduwa  wake zao waja wazito ni vizuri kuwasindikiza hospitali kupata pamoja elimu ya afya ya uzazi na kufahamu athari za kuchelewa kuhudhuria kliniki mapema.

Vile vile wanatoa ushauri kupitia ujumbe ama taaluma kutoka kwa madaktari ili kulea familia yake na kupata muda wa kufanya majukumu yake kwa kupanga uzazi.

Daktari bingwa wa magonjwa ya wanawake na uzazi kutoka Hospirali ya Rufaa Mnazi Mmoja, Ummulkuthum Omar, alisema wanatoa taaluma kwa mama wajawazito kuhudhuria kliniki mapema wakati wakigunduwa tu wameshashika ujauzito ili kuepuka athari.

“Tunawahamasisha mama waja wazito kufika kliniki kuanzia wiki moja ya ujauzito lakini  baadhi yao ni wakaidi  na wanakuja mimba ikiwa ni ya miezi mitano mpaka sita.

Akiwa na tatizo, basi hali huwa ngumu kidogo kuishughulikia,” alifafanua Dk Ummulkulthum Kwa mujibu wa Takwimu mama  wajawazito waliohudhuria klinikic mapema  kutoka Kituo cha Afya cha Mwera 2020/2021 ni 147 ambapo kwa mwaka 2022/2023 kuanzia January hadi Augosti 150.

 

 

   

MIKAKATI YA WIZARA YA AFYA ZANZIBAR

Katika hotuba yake ya bajeti ya 2021/22, Waziri wa Afya, Ustawi wa Jamii, Wazee, Jinsia na Watoto Zanzibar, Mh. Nassor Ahmed Mazrui,   alisema katika kuhakikisha vifo vya mama wajawazito vinapunguwa Wizara  inafanya juhudi mbali mbali zae  kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi.

Miongoni mwa juhudi hizo ni kuhakiki vifo ili kubaini sababu zilizopelekea kutokea na kuchukua hatua stahiki.

Katika kipindi cha Julai 2020 hadi Machi 2021, vifo vya mama 44 na watoto wachanga 1,201 viliripotiwa katika hospitali zinazotoa huduma za uzazi.

Vifo vya mama ni 28 (asilimia 63) na vya watoto wachanga 446 (asilimia 37) vilihakikiwa. Matokeo ya uhakiki huo yamebainisha sababu za vifo ni pamoja na watoto kukosa hewa wakati wa kuzaliwa; uzito pungufu; njiti; kupoteza damu na maambukizi kwa watoto wachanga.

 Kwa upande wa vifo vya mama ni kifafa cha mimba, upungufu wa damu wakati wa ujauzito, kupoteza damu wakati wa ujauzito, kisukari na maradhi mengine sugu wakati wa ujauzito.

  Ingawa jitihada zinafanywa na Wizara husika ya kuwahamasisha akina mama wajawazito kuhudhuria kliniki  bado elimu ya ziada inahitajika.

Takwimu za Wizara ya Afya, Jinsia, Wazee na Watoto Zanzibar zinaonesha mama wajawazito 46,050 walihudhuria kliniki ya upimaji mimba angalau mara moja katika kipindi cha ujauzito kwa mwaka 2020/2021 ukilinganisha na 40,177 wa mwaka 2019/2020.

 Katika kipindi hicho, akina mama waliojifunguwa walikuwa ni 33,057,  sawa na asilimia (61.3%) Kwa hospitali za Unguja ni Unguja ni 22,164 na Pemba ni 10,893.

Mradi wa Afya ya Uzazi Wasichana  na Wanawake umefadhiliwa na Shirika la Wellspring Philanthropic Fund la Marekani.

Kwa sasa mradi huu unatekelezwa na Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake kwa Upande wa Bara na Zanzibar kwa lengo la kuongeza ushawishi na utetezi kwa kupitia vyombo vya habari juu ya umuhimu wa upatikanaji wa huduma ya Afya ya Uzazi kwa wasichana na wanawake

Post a Comment

0 Comments