Ticker

6/recent/ticker-posts

Sharia Mpya Ya Habari Kilio Kisicho Na Majibu Kwa Miongo Miwili

 


Na Ahmed Abdulla, Zanzibar:

Kwa zaidi ya miongo miwili, wadau wa habari visiwani Zanzibar wamekuwa wakidai kwa nguvu sheria mpya ya habari itakayokuwa rafiki kwa vyombo vya habari na kulinda haki ya kupata taarifa.

Licha ya ahadi nyingi kutoka kwa viongozi wa serikali, sheria hiyo bado haijafika mezani mwa Baraza la Wawakilishi hali ambayo inaibua maswali kuhusu dhamira ya kweli ya kutaka kulinda uhuru wa habari na kuchochea utawala bora.

Katika tukio muhimu la mwaka 2022 Pale Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi alipokutana na Waandishi wa Habari, alikiri bayana kuwa sheria za habari za Zanzibar zimepitwa na wakati na hazina ufanisi unaotakiwa katika mazingira ya sasa ya kidemokrasia.

“Sheria za habari za Zanzibar ni za muda mrefu, na Serikali anayoiongoza ipo tayari kushirikiana na wadau wa habari kuzifanyia kazi kulingana na mapendekezo yatakayotolewa,” alisema Rais Mwinyi, na kuongeza: “Pendekezo lenu la kwamba Zanzibar imefika wakati wa kupata sheria nzuri, tutalifanyia kazi.”

Kauli hiyo iliongeza matumaini katika mioyo ya wanahabari na watetezi wa haki za binadamu, lakini hatua za utekelezaji zinaendelea kuwa za kusuasua.

Katika kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari duniani, Mei 3, 2023, yaliyofanyika katika Ukumbi wa Hoteli ya Golden Tulip, Uwanja wa Ndege Rais Mwinyi aliendeleza msimamo wake wa kuunga mkono uhuru wa vyombo vya habari.

“Serikali zote mbili zitaendelea kushirikiana kwa karibu na vyombo vyote vya habari katika kuhakikisha changamoto zinazowakabili wanahabari zinatatuliwa,” aliahidi Rais huyo mbele ya wanahabari, wanaharakati na viongozi wa serikali.

Ahadi hiyo ilirudiwa na Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Tabia Maulid Mwita, ambaye alitangaza kuwa mchakato wa maandalizi ya sheria mpya ya habari ulikuwa umefikia asilimia 80.

“Serikali yenu ni sikivu. Tunawahakikishia kuwa na sheria nzuri zitakazokidhi matakwa ya sasa. Tutaiwasilisha Baraza la Wawakilishi na taratibu nyingine ziendelee,” alisema Waziri Tabia huku akiwasihi wadau kuwa na subira.

Aidha, Waziri huyo aliongeza matumaini kwa kusema:

“Tuna Baraza la Mapinduzi na tunategemea kwenda kuisoma sheria yetu mpya ya habari na tutaipeleka Baraza la Wawakilishi ambako matarajio ni kutungwa na kuwa sheria mpya,” alieleza Tabia Maulid Mwita, akiashiria kuwa mchakato huo uko hatua za mwisho kabla ya kuwasilishwa rasmi.

Mwandishi Mkongwe wahabar ambaye pia ni Mwalimu wa Uandishi wa Habari Tanzania na Afrika Mashariki, Salim Said Salim alisema demokrasia sahihi hutegemea kwa kiasi kikubwa uhuru wa vyombo vya habari katika nchi, kwa sababu vyombo vya habari vina dhima ya kuchangia maendeleo ya nchi kwa kupaza sauti na kuwawajibisha viongozi wanaotumia mamlaka kinyume cha sheria.

“Hii Sheria ya Habari ina miaka takriban 20 sasa tokea kuanza kuilalamikia, tunapewa ahadi kila siku lakini bado hatujaona utekelezaji wake. Kama ni mtoto tayari angekuwa anasoma chuo kikuu,” anasema veterani aliyeanza kuwa mwandishi wa habari mwaka 1965.

Kwa upande wa Muandishi nguli wa habari Viziwani Zanzibar Salum Vuai alisema kwa msisitizo “Chombo cha habari kinaandika na kutangaza ikiwa ni pamoja na kufichua baadhi ya maovu, jambo ambalo baadhi ya viongozi hawapendi hivyo afisa wa polisi anaweza kutumia fursa hiyo kwenda kukamata gazeti; hii haingii akilini katika ulimwengu huu wa utandawazi”

Amour Khamis ni Mhariri wa  Zanzibar Cable TV alisema uwepo sharia zisizorafiki katika uhuru wa habari kunapelekea waandishi washindwe  kuandika habari zinazokosoa mamlaka au watu waliopewa mamlaka jambo linaloweza kuondosha utawala bora nchini.

“Kwa mara nyingi hutumika neno ‘maslahi ya umma’ bila kufafanua ni yapi hayo maslahi ya umma, tunaweza kuingizwa hatiani kwa kutumia  haya maneno yaliyopo kwenye vifungu vya sharia zetu za habari hivyo hapa dhana ya utawala bora inaweza kupotea” alisema Amour

Afisa Programu kutoka chama cha waandishi wa habari wanawake Zanzibar Zaina Mzee alisema taifa haliwezi kupata maendeleo ya haraka kukiwa hakuna sharia bora zinazowapa uhuru waandishi wa habari.

“Maendeleo ya haraka haji hivihivi pasi na kuwa na sharia bora ya habari inayotulinda sisi wanahabari.” Alisema

Mfano wa sharia hizo ni Sheria ya Tume ya Utangazaji No. 7 ya 1997 kama ilivyofanyiwa marekebisho na sheria No. 1, 2010 kifungu cha 27 (2).

alisema kuwa Kifungu hiki kimempa Waziri mamlaka makubwa ya kuchukua maamuzi yoyote kwa chombo cha utangazaji ikiwa kimetangaza jambo lolote kinyume na usalama wa taifa na maslahi yaumma.

Post a Comment

0 Comments