Ticker

6/recent/ticker-posts

Mchango Wa Sheria Katika Kuendeleza Sekta Ya Habari Na Kuleta Mabadiliko Ndani Ya Nchi.

 


Na Siti Ali, Zanzibar:

Sekta ya habari kwa kiwango kikubwa kina mchango mkubwa  katika jamii kwenye kuleta mabadiliko na maendeleo  ,haki na wajibu lakini pia inashughulikia tatizo kubwa la hadhi ya wanahabari ambayo ni kuifanya kazi ya habari iwe taaluma ambayo kipato chake kinaelezeka kwa mujibu wa sheria.

Sheria  pia ina mchango mkubwa katika sekta ya habari kwani imetoa fursa na uhuru kwa kila mtu kujieleza,kutoa taarifa ,kupokea taarifa,kulingana na katiba ya jamuhuri ya muungano wa tanzania  (ibara ya 30 na ibara ndogo ya 5) ambayo inasema furahiya haki zako lakini usiharibu amani,maadili usalama wa watu pamoja na maslahi ya umma,hii inatokana na uhuru wa kujieleza kwa kufuata sheria zinazowaongoza wanahabari.

Taasisi za kimataifa ambazo zinafanya tathmini ya hali ya kidemokrasia ,uhuru wa habari na kujieleza ,zinatumia taarifa za sasa baada ya mabadiliko na kufanya tathmini.

Maana wamekuwa wakitumia taarifa za muda mrefu na kuifanya nchi kuonekana imepiga hatua katika  sheria ya habari,uhuru  wa wanahabari na kutanua wigo wa demokrasia.

Licha ya kuwepo mafanikio mbali mbali ya sheria katika sekta ya habari lakini pia zipo changamoto za sheria ambazo zinaikabili sekta ya habari ambazo zinarudisha nyuma uhuru wa habari kama ifuatavyo :

Sheria ya uhuru wa habari zanzibar katika katiba ya mwaka 1984 kama inavyosomeka  ibara ya 18 (1)Bila ya kuathiri sheria nyengine za nchi,kila mtu anayo haki ya uhuru wa maoni (kujieleza),kutafuta,kupokea na kusambaza habari na mawazo yake kupitia chombo chochote cha habari bila ya kujali mipaka ya nchi na pia anayo haki na uhuru wa kutoingiliwa mawasiliano yake. Ambapo sheria hii inampa mwandishi wa habari fursa ya kutoa na kusambaza ujumbe kwa jamii ikiwa ndio lengo halisi la mwandishi wa habari.

Sheria nyengine ni sheria ya Tume ya Utangazaji na.7 ya mwaka 1997 iliyofanyiwa marekebisho na sheria na.1 ya Mwaka 2010.ambapo sheria hii inampa fursa ya mwandishi wa habari kufanya kazi lakini pia sheria hii sio rafiki kwani haimlindi mwandishi wa habari katika kazi yake.

Sheria ya Wakala wa Usajili wa Wakala wa Habari, Magazeti na Vitabu na.5 ya mwaka 1988 iliyofanyiwa marekebisho na sheria na.8 ya mwaka 1997.ambapo pia sheria hii licha ya kufanyiwa marekebisho lakini pia ina mapungufu ambayo yanamuathiri  mwandishi wa habari katika kufanya majukumu yake ya kila siku,ni vyema mamlaka husika kulifanyia kazi suala hili kwa haraka ili kumaliza kilio cha waandishi wa habari.

Mwandishi wa habari kutoka gazeti la Chanzo  Najjat  Omar amesema kuwa sheria ya habari ina mchango mkubwa katika kuleta miongozo na kufuata mambo mbali mbali ingawa bado zipo sheria ambazo zimekuwa na changamoto nyingi ambazo zinamkwaza mwandishi wa habari katika kutekeleza majukumu yake ya kila siku.

“Sheria ina mchango mkubwa katika kuleta mabadiliko katika nchi kwani nchi yoyote haiwezi kwenda bila ya sheria ambayo inatoa miongozo mbali mbali hivyo natoa wito kwa Serikali isikilize kilio cha waandishi wa habari kuupitisha muswaada wa sheria ili kupata unafuu mkubwa katika kuisadia Serikali kuleta demokrasia na amani ya nchi”ameelezea Najjat  Mwandishi wa habari

Mwandishi wa habari wa kujitegemea  Ali Vuai Kombo,anasema kuwa  sheria ya habari ina mchango mkubwa katika kusimamia majukumu ya wanahabari na utekelezaji wa muandishi wa habari kwenye kazi zake pamoja na kulinda haki za jamii kupitia vyombo vya habari hivyo ni wazi kuwa mchango wa sheria ni mkubwa kulingana na maendeleo yaliopo katika nchi.

“Mchango wa sheria ni mkubwa kulingana na mabadiliko ya nchi kwani mwandishi wa habari anatakiwa kufuata maadili yake ambayo ni kama sheria itakayo muwezesha kufanya majukumu yake ya kila siku ambayo yanamsaidia kuleta maendeleo katika nchi na taifa kwa ujumla”amesema Ali Vuai.

Mwanasheria Juma Khamis Juma amesema kuwa sheria ina mchango mkubwa katika sekta ya habari kwani ni muhimu katika maendeleo ya nchi,pia na kusema kuwa nchi yenye sheria sio tu ya habari bali hata sheria nyengine ndiyo yenye nafasi ya kupiga hatua mbele katika kuleta mabadiliko na maendeleo.

“Sheria ina mchango mkubwa katika sekta ya habari kwani ni muhimu katika maendeleo ya nchi,kwani nchi yenye sheria sio tu ya habari bali hata sheria nyengine ndiyo yenye nafasi ya kupiga hatua mbele katika kuleta mabadiliko na maendeleo”anaelezea Mwanasheria Juma.

Licha ya kuwepo kwa changamoto mbali mbali zinzogusa sheria ya habari hapa Zanzibar lakini bado kuna hatua tofauti zinazochukuliwa na Serekali katika kutatua kilo cha waandishi wa habari cha kulipitisha sheria mpya ya habari ambayo inakwenda kuikomboa sekta ya habari na uhuru wa habari.

Waziri wa Habari Vijana Utamaduni na Michezo Mh Tabia Maulid Mwita wakati akizungumza na Maafisa habari tarehe 4 aprili katika ukumbi wa New Amani Comples amesema katika kipindi kijacho Serikali inatarajia  kuisoma pamoja na kuipitisha sheria ya habari ambayo itasaidia kuleta mabadiliko katika nchi na taifa kwa ujumla.

“Kipindi kijacho Serikali inatarajia  kuisoma pamoja na kuipitisha sheria mpya ya habari ambayo itasaidia kuleta mabadiliko wanahabari pamoja na taifa kwa ujumla”ameelezea Waziri Tabia.

Katibu wa Clabu ya waandishi wa habari zanzibar (ZPC)Mwinyimvua Abdi Mzukwi amesema kuwa sheria ya habari ina mchango mkubwa kwani inasaidia kuongeza uwajibikaji kwa waandishi pamoja na kulinda maslahi mwandishi.

“Sheria ikiwa rafiki kwa waandishi kutapelekea kuongeza ari na mori kwa waandishi kufanya kazi kwa bidii pamoja na kuwajibika ipasavyo kwenye majukumu yao kwani kufanya hiivyo kutapelekea kupata mabadiliko katika sekta ya habari na maendeleo katika nchi”Mwinyimvua anaeleza.

Afisa Program kutoka Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA -ZNZ) Zaina Abdallah Mzee anasema kuwa sheria zilizopo zikifanyiwa marekebisho na zitaweza kuondoa woga kwa waandishi wa kukusanya na kuripoti habari na kuiwezesha jamii kupata taarifa kwa wakati .

“Kwa kipindi kirefu tumeendelea na kufanya uchechemuzi lakini marekebisho ya sheria kuu mbili yaani Sheria ya Wakala wa Habari Magazeti na Vitabu ya Mwaka (1988)na sheria ya Tume ya Utangazaji Zanzibar  ya mwaka (1997)ambazo waathirika wakubwa ni waandishi,vyombo vya habari  na jamii  iliyotuzunguka “ameeleza Afisa huyo.

Kwa ujumla sheria ina mchango mkubwa katika kuendeleza sekta ya habari na kuleta mabadiliko katika nchi, kwani Mwandishi wa habari akifuata maadili ya uwandishi wa habari ataweza kufanya kazi zake bila ya kupata usumbufu katika kazi zake.

Hivyo ni vyema kwa waandishi wa habari kufuata sheria na maadili  katika kazi zao ambazo zitawasaidia katika kutatua migogoro binafsi na kuleta maslahi ya taifa.

 

 

Post a Comment

0 Comments