Thuwaiba
Habib, Zanzibar:
Muhitaji hachoki ni msemo wa Kiswahili uliotumiwa sana
kipindi cha nyuma na watu walipokuwa wakisaka maendeleo ya nchi.
Na kwa kuwa watu wote walikuwa na nia ya dhati ya
kulifanikisha hilo kwa kiwango kikubwa basi liliwezekana.
Vile vile msemo huo ulibainika tena
mwaka 2023 baada ya wadau wa masuala ya habari kujikusanya na kuangalia
mapungufu yaliyomo ndani ya sheria ya habari ambayo ina kandamiza uhuru wa
habari na kujieleza na kutaka kuona mwafaka wa sheria hiyo hapa Zanzibar.
Mwandishi wa habari kutoka Zenji Fm Berema Suleiman
anasema kuchelewesha kwa mchakato wa kuundwa kwa sheria mpya na rafiki za
habari visiwani Zanzibar kunasababisha hofu kwa waandishi na vyombo vya habari,
kunadumaza demokrasia na utawala bora.
"Nchi ambayo haina sheria rafiki za vyombo vya
habari inaweza kuchelewa kupata maendeleo kwa sababu changamoto zinazowakabili
wananchi haziwezi kuibuliwa na kufika kwa haraka kwa mamlaka," anasema
Berema.
Mwandishi wa habari
wa gazeti la Mwananchi Jesse Mikofu anasema Mchakato wa
kuundwa kwa sheria mpya unachelewesha upatikanaji wa uhuru wa habari kwa sababu
dana dana za kufanyiwa kazi jambo hilo zimekuwa nyingi kwani ni zaidi ya miaka
20 jambo hilo linazungumzwa na ufumbuzi haujapatikana.
"Suala hili linachelewesha uhuru wa habari
kwasababu sheria rafiki haipo na sheria ndio inayoongoza kila kitu na kama huna
sheria mzuri huwezi kufanya kitu kizuri kutokana na kuwapo sheria inayowabana
waandishi ndiyo utendaji kazi wao unapopungua kasi"
Katibu Mkuu wa Zanzibar Press Club (ZPC) Mwinyimvua
Abdi Nzukwi anasema kitu kikubwa ambacho pia kinahamasisha waandishi kutaka
sheria mpya kwa haraka ni kupitiwa na wakati kwa sheria hii ya Usajili wa
Wakala wa Habari, Magazeti na Vitabu ambayo imetungwa mwaka 1988 kufanyiwa
marekebisho madogo 1997.
"Ni muhimu sheria ya habari rafiki ipatikane na
iweze kuendana na mazingira ya sasa ambayo haitakuwa na vithibiti vingi vinavyokwaza
uhuru wa habari na wa kujieleza"
Kutokana na ahadi mbali mbali kutoka serikalini moja
ya kauli kutoka kwa kiongozi ilisema ya kuwa sheria habari zipo kwa makatibu wakuu na zinafanyiwa kazi.
Waziri ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo wa Zanzibar
Tabia Mwita aliwapa matumaini wanahabari kwenye mahojiano maalum hivi karibuni
kwamba tayari vikao na wadau vimeshafanyika kuhusu sheria hizo na kwamba kwa
sasa Serikali iko kwenye hatua ya mwisho ya mchakato wa maboresho ya sheria
husika.
Serikali imepokea maoni ya wadau na muswada [wa
marekebisho ya sheria] upo katika ngazi ya Makatibu Wakuu, Tabia alisema kwenye
mahojiano hayo. Hivyo, kama Serikali tunajitahidi kuweka mazingira rafiki kwa
waandishi ili waweze kufanya kazi zao kwa weledi.
Mwanasheria na Mtetezi wa masuala ya Habari, Juma
Khamis Juma anasema Mchakato wa sheria mpya ya habari ulianza zaidi ya miaka 20
iliyopita. Wadau mbalimbali kwa kushirikiana na Baraza la Habari Tanzania,
walianzisha mchakato huu kwa pande zote mbili za Muungano, lakini wenzetu
Tanzania Bara wakafanikiwa kupata sheria ya Huduma za Habari mwaka 2016.
" Ingawa ina kasoro za msingi lakini angalau kuna
sheria mpya. Kwa upande wa Zanzibar juhudi mbalimbali zimechukuliwa na wadau,
lakini hadi sasa bado sheria mpya haijapatikana.
“Upande wa Serikali unaeleza hatua inazochukua
kuhakikisha sheria mpya inapatikana lakini wadau wanaona hatua bado ni za
kusuasua, lakini naamini siku moja tunaweza kuwa na sheria bora ya habari
itakayokata kiu ya kila mdau,” anasema Juma.
Mkurugenzi wa Chama cha Waandishi wa Habari Tanzania,
Zanzibar (TAMWA - ZNZ), Dkt. Mzuri Issa anasema mchakato wa mabadiliko ya
sheria za habari umekuwapo kwa miaka mingi lakini bado sheria hizo ambazo
nyingi ni za muda mrefu zimekwama kurekebishwa.
Sisi wengine tangu tuko waandishi chipukizi
tunazungumzia kupata hizi sheria mpya za habari, tangu 2008 kwa kweli ni muda
mrefu, tunahitaji kusimamia jambo hili kwa umoja wetu na hatimaye tupate sheria
mpya
Serikali visiwani hapa imebainisha kwamba inayasikia
malalamiko ya wadau wa habari kuhusu uwepo wa sheria kandamizi za habari na
zilizopitwa na wakati, ikisema kwamba iko mbioni kuzifanyia maboresho sheria
hizo.
Afisa Programu wa TAMWA ZNZ, Zaina Mzee, amewataka
wanahabari kuendelea na harakati za kutaka kuwapo kwa sheria mpya rafiki za
habari. “Sheria hizi si tu zitahakikisha uhuru wa kujieleza bali pia
zitaimarisha utoaji wa huduma za jamii na maendeleo kwa ujumla,” anasema Zaina.
0 Comments