Ticker

6/recent/ticker-posts

FAWE Zanzibar Yajidhatiti Kutoa Elimu Ya Jinsia

 


JUKWAA la walimu Wanawake wa kiafrika upande wa Zanzibar  (FAWE-ZNZ) limesema litaendelea kutoa elimu ya jinsia kwa walimu kwasababu bado baadhi yao hawana uelewa wa kuwasaidia watoto pale wanapokuwa katika majukumu yao ya kazi.

Mjumbe wa Bodi ya FAWE Zanzibar Khadija Bakar Juma alisema hayo alipokuwa akifunga mafunzo ya kuwajengea uwezo namna bora ya ufundishaji unaozingatia jinsia kwa wanafunzi wanaosoma kada ya Ualimu kutoka Chuo cha Kiislam Zanzibar.

Alisema hatua hiyo itasaidia walimu kuwaelewa wanafunzi na kuweka ustawi mzuri wa watoto hao na kufikia ndoto zao.

Mjumbe huyo alifahamisha kuwa ni vyema walimu kujifunza usimamizi wa mabadiliko ya wanafunzi katika ukuwaji wao, mahusiano baina ya walimu na wanafunzi ili kujua tabia za wanafunzi wakati wakiwa darasani.

Aidha aliwataka wanafunzi hao kuongeza matumizi ya lugha katika masomo yao na kujifunza dhana za kufundisha ili kutekeleza vyema majukumu yao kwasababu uzoefu unaonesha kwamba baadhi ya wanafunzi wanapokuwa skuli hukabiliwa na vikwazo mbalimbali na kushindwa kumudu vyema masomo yao.  

Mbali na hayo alitumia fursa hiyo kuwataka mafunzo walioyapata kwenda kuwafundisha na wenzao ili elimu hiyo iwafikie watu wengi na kuweza kuweka ustawi mzuri wa watoto na taifa kwa ujumla.

Kwa upande wake Mratibu wa FAWE Zanzibar Winnifred Yatuwa Mamawi alisema mradi wa ufundishaji unaozingatia jinsia ni mradi wa majaribio unaotekelezwa na FAWE Unguja na Pemba kwa lengo la kuondosha matukio ya udhalilishaji katika skuli.

Nae Martin Okhako kutoka FAWE Nairobi alisema wameona kunahaja kubwa ya kuelekeza mradi huo kwa walimu kwa lengo la kuleta mabadiliko katika ufundishaji wao.

Mkufunzi wa Mafunzo hayo Neema Kitundu kutoka FAWE Tanzania bara alisema walimu wanadhamana kubwa ya kuhakikisha wanasimamia wanafunzi wakati wakiwa darasani, hivyo wanawajibu wa kuendeleza ujuzi zaidi ili kupata mbinu bora za kufundisha.

Kwa upande wa wanafunzi hao walisema mafunzo hayo yamewafunda baadhi ya matendo ambayo hawakujua kama ni udhalilishaji, hivyo waliahidi kuyatumia vyema mafunzo waliopatiwa pale wanapotekeleza majukumu yao ili kuweka mustakabali mwema kwa wanafunzi na kuchochea maendeleo yao.

Mafunzo hayo ya siku nne yameandaliwa na FAWE Zanzibar ikiwa ni moja ya utekelezaji wa mradi wa kukuza ubora wa elimu kwa watoto wa kike unatekelezwa na FAWE Zanzibar.

 

Post a Comment

0 Comments