Takriban zaidi ya miaka 10 sasa wadau wa habari
na waandishi wa habari Zanzibar wanalilia mabadiliko ya sheria za habari ambazo
ndani yake kuna vifungu vinavyokwaza na kuminya uhuru wa habari nchini.
Wadau hao wakiwemo Chama cha Waandishi wa Habari
Tanzania Zanzibar (TAMWA-ZNZ), MCT, WAHAMAZA, ZPC hawajakata tamaa katika
kufanya uchechemuzi kwa lengo la kupata kile ambacho wanahisi kitakuwa mkombozi
katika tasnia yao.
Hamasa ya kuripoti na kuandika taarifa zinazohusu
umuhimu wa uhuru wa habari, uhuru wa kupata taarifa na uhuru wa kujieleza
kwa waaandishi na vyombo vya habari ndio kipaombele kikubwa ambapo kwa sasa umuhimu huo unaonekana kwa
asilimia ndogo katika visiwa vya Zanzibar.
Mkurugenzi wa Chama cha Waandishi wa Habari
Wanawake Tanzania, Zanzibar (TAMWA ZNZ), Dkt. Mzuri Issa, amehimiza vyombo vya
habari kuripoti kwa kina mapungufu ya sheria za habari za Zanzibar ili
zifanyiwe marekebisho na kutoa fursa kwa wananchi kupata habari bila vikwazo.
"Waandishi wa habari tutumie nafasi kupaza
sauti zetu juu ya mapungufu ya kisheria yaliyopo ili zifanyiwe marekebisho, hii
itawapa watu furaha na kujisikia kuwa ni sehemu ya nchi kwa kutoa maoni yao
bila hofu,” alieleza Dkt. Mzuri.
Alibainisha kuwa waandishi wa habari wakiwa na
uwezo wa kutoa maoni yao bila hofu itarahisisha upatikanaji wa taarifa na
kuongeza uwajibikaji katika nyanja mbalimbali.
"Kukiwa na uhuru wa habari itasaidia
kupunguza madhaifu yaliyopo kwenye sekta ya habari kwa kudhibiti waandishi
holela wanaotoa taarifa feki na kuifanya sekta ya habari kuwa imara na kutoa
taarifa ambazo zinakidhi misingi ya uandishi." Alieleza.
Kwa upande wake mkufunzi wa Chuo Kikuu cha
Zanzibar Said Suleiman Ali ambae pia ni mchambuzi wa sheria mbali mbali za
habari wa habari alisema uchambuzi wa sheria hizo umebaini kuwepo baadhi ya
vifungu vinavyokwaza uhuru wa habari.
Aliongeza kuwa ripoti hiyo imepitia jumla ya
sheria nane (8) ambazo ni Sheria ya usajili wa wakala wa habari, magazeti na
vitabu namba 5 ya mwaka 1988 iliyofanyiwa marekebisho na sheria no.8 ya 1997,
Sheria ya Tume ya Utangazaji Zanzibar namba 7 ya mwaka 1997 iliyorekebishwa na
sheria namba 1 ya mwaka 2010.
Nyengine ni sheria ya Adhabu ya Mwaka 2004
(Sheria Na. 6) iliyorekebishwa mwaka 2018, Sheria ya kufuta Sheria ya Uchaguzi
Na. 11 ya mwaka 1984 na kutungwa kwa Sheria ya Uchaguzi ya mwaka 2017 na mambo
mengine yanayohusiana na hayo pamoja na Sheria ya Baraza la Wawakilishi Na 4 ya
mwaka 2007 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2022.
Alieleza kuwa Sheria ya Tume ya Utangazaji Na. 7 ya 1997 kama ilivyofanyiwa marekebisho na sheria Na. 1, 2010 inahitaji kufanyiwa marekebisho kifungu cha 27 (2) kutokana na kutoa mamlaka zaidi kwa viongozi.
"Sheria ya Tume ya Utangazaji No. 7 ya 1997
kama ilivyofanyiwa marekebisho na sheria No. 1, 2010 viongozi wamepewa mamlaka
makubwa sana mfano kifungu cha 27 (2). Waziri amepewa mamlaka makubwa sana ya
kuchukua maamuzi yoyote," alieleza mkufunzi huyo.
Alipendekeza sheria na sera kuwekewa vifungu
vinavyoweka mazingira ya usalama wa waandishi wa habari ili kuwalinda dhidi ya
uvunjifu wa uhuru wa kujieleza.
Alisema, "Sera na sheria lazima zihusishe
vifungu vinavyohakikisha usalama wa waandishi wa habari, wanaharakati na
wasomaji ili kuwaweka katika mazingira salama."
Mratibu wa program ya kuendeleza mapitio ya uhuru wa Sheria za
habari (ARFEL), Zaina Mzee, alisema ipo haja ya kufanyiwa marekebisho kwa
sharia hizo hususan mama za habari ili kupata sheria rafiki na zenye muktadha mwema
wa tasnia ya habari.
“Ipo sheria ya Tume ya Utangazaji Zanzibar
nambari 7 ya mwaka 1997, 1997 iliyorekebishwa na
sheria namba 1 ya mwaka 2010, pamoja
na sheria nambari 5 ya Wakala wa
Habari, Magazeti na Vitabu ya mwaka 1988 iliyofanyiwa marekebisho na sheria no.8 ya 1997.
Alisema sheria hizo, zimekuwa na
vifungu ambavyo sio rafiki kwa kuimarisha uhuru wa habari pamoja na uhuru wa kujieleza
katika jamii.
Sambamba na hilo mratibu huyo
aliongezea kuwa pamoja na ukongwe wake sheria hizo mbili kuu zinazosimamia
vyombo vya habari, lakini kubwa zaidi zimekuwa zikiwabana waandishi katika
kutekeleza haki yao ya kikatiba.
‘’Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984,
kwenye kifungu chake cha 18 kimeweka wazi suala la kupata, kusambaaza habari
habari tena bila ya kujali mipaka ya nchi,’’anasema ilivyoeleza sehemu ya
katiba.
Jabir Idrissa, ambaye ni mdau wa habari alisema,
uwepo wa sheria zinazokwaza uhuru wa habari imepelekea Zanzibar kukosekana kwa
vyombo vya habari binafsi kwa upande wa magazeti kutokana na urasimu katika
utekelezaji wa sheria hizo.
"Mpaka leo Zanzibar hakuna Gazeti binafsi,
ambapo kabla ya Mapinduzi kulikuwa na magazeti mengi Zanzibar, historia ya
uandishi wa habari Zanzibar ni ya muda mrefu lakini imekufa kutokana na uwepo
wa sheria zisizo rafiki," alieleza mdau huyo.
Nae Mratibu wa MCT-Zanzibar Shifaa Said amesema wakati umefika
sasa kwa waandishi wahabari kutumia vyema kalamu zao kuikumbusha
Serikali namna gani sheria zilizopo zinavyoathiri uhuru wa kutoa na
kupata habari nchini .
“Ni wakati sasa waandishi wa habari kutumia kalamu zenu kuonesha
kwa namna ambavyo sheria zilizopo zinavyoathiri tasnia ya habari na zinahitaji
kufanyiwa marekebisho kwa maslahi ya umma”, alisema Shifaa Said.
Mwandishi mwandamizi kutoka Zanzibar Salim Said Salim amesema ni
Utamaduni wa watu wa Zanzibar ulianzia enzi za kale kupenda kupokea habari
kupitia njia tofauti hivyo ni vyema kuendelezwa bila ya vikwazo kupitia sheria
za habari.
“Wazanzibar walipenda kupata habari kama njia moja ya
mawasiliano kupitia njia tofauti, tukiwa kwenye usafiri wa baharini (meli)
kulikuwa na vipaza sauti (mabomba)
ambayo yanatowa taarifa za habari na abiria wakipata kujua kila kilichokuwa kinaendelea/
kinatokea kwa wakati huo,” Salim Said.
Mradi wa kuimarisha masuala ya uhuru wa habari ni wa miaka
miwili wenye lengo la kuendeleza mapitio ya uhuru wa Sheria za habari (ARFEL), ambao
unatekelezwa na TAMWA-ZNZ kwa kushirikiana na Commonwealth Foundation.
0 Comments