Ticker

6/recent/ticker-posts

Hali Ya Vyombo Vya Habari Zanzibar Yatia Huzuni



Na Mwandishi Wetu:

Jioni wa tarehe 26 Oktoba 2015, hewani kupitia redio ya kijamii Swahiba FM ya Zanzibar, kulisikika sauti ya Maalim Seif Sharif Hamad, aliyekuwa mgombea urais kupitia Chama cha Wananchi (CUF), akizungumza moja kwa moja na waandishi wa habari.

Katika mkutano huo uliopeperushwa moja kwa moja, Maalim Seif alitangaza kuwa kwa mujibu wa takwimu zilizokusanywa na mawakala wa chama chake kutoka vituo vya kupigia kura, alikuwa ameshinda urais wa Zanzibar kwa asilimia 52.87, dhidi ya Rais aliyekuwa madarakani kwa tiketi ya CCM, Dk. Ali Mohamed Shein, aliyepata asilimia 47.13, katika uchaguzi uliofanyika Oktoba 25, 2015.

Swahiba FM, ikiwa ni chombo cha habari kilicho karibu na wananchi, ilikusudia kuwapatia taarifa mapema juu ya kinachoendelea, kama sehemu ya wajibu wake wa kuhudumia umma.

Lakini ndani ya saa chache, hali ilibadilika. Tume ya Utangazaji Zanzibar (ZBC) iliamuru redio hiyo ifungwe mara moja, kwa madai ya "kurusha taarifa zisizothibitishwa rasmi na Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC)." Redio hiyo ilishtumiwa kwa "kujitangazia matokeo," jambo lililoonekana kuwa kinyume cha sheria za uchaguzi za wakati huo.

Tukio hili lilisababisha mjadala mkubwa kitaifa na kimataifa kuhusu uhuru wa habari wakati wa chaguzi, mipaka ya vyombo vya habari, na mazingira ya kisheria yanayowakabili wanahabari Zanzibar.

Mashirika ya haki za binadamu na watetezi wa uhuru wa vyombo vya habari walihoji:

"Je, ni sahihi kwa chombo cha habari kufungiwa kwa kurusha matamko ya mgombea? Je, sheria zetu zinawalinda waandishi au zinawatisha?"

Kwa waandishi wa habari na wachambuzi wengi, kufungiwa kwa Swahiba FM kilikuwa kielelezo cha wazi cha udhaifu wa mfumo wa kisheria katika sekta ya habari.

Tukio hilo lilionyesha bayana hitaji la dharura la sheria mpya ya habari sheria itakayolinda uhuru wa kujieleza, kuimarisha uwajibikaji, na kulinda tasnia ya habari dhidi ya ukandamizaji wa kisiasa.

Kutokana na mkasa huo na mengine mingi kwa wanahabari na vyombo vya habari kuwa na hofu juu ya uhuru wao kwenye tasnia hiyo zaidi ya miaka ishirini, wadau wa sekta ya habari visiwani Zanzibar wamekuwa wakihimiza kupitishwa kwa sheria mpya ya habari.

Licha ya mazungumzo, semina, na ahadi kutoka kwa viongozi wa serikali, bado hakuna utekelezaji wa dhati uliofanyika. Ukosefu huu wa sheria umeendelea kuathiri kwa kiasi kikubwa utendaji wa vyombo vya habari na namna taasisi za serikali zinavyowajibika kwa umma.

 

Hofu ya kufanya kazi kwa waandishi wa habari inaweza kusababibsha kutokuwepo kwa utawala bora kwama anavyoeleza Warda Khatibu Khamis, Katibu wa Jumuiya ya Kijana Amka Wajibika, "Kukosekana kwa sheria bora ya habari kunachangia kwa kiasi kikubwa ukosefu wa uwajibikaji kwa taasisi za serikali na vyombo vya habari vyenyewe."

Mkurugenzi wa Chama Cha Waandishi wa Habari Wanawaeke Tanzania upande wa Zanzibar Dklt. Mzuri Issa anasema Sheria zilizopo hivi sasa zinatoa mamlaka makubwa kwa viongozi wa serikali kuingilia uhuru wa vyombo vya habari.

"Kifungu cha 30 cha Sheria ya Wakala wa Habari, Magazeti na Vijarida Na. 5 ya 1988 kinampa Waziri mamlaka ya kufungia gazeti kwa kigezo cha 'maslahi ya taifa'. Mamlaka haya yanaweza kutumiwa vibaya kisiasa."

Jabir Idrissa, mwandishi wa muda mrefu na mdau wa habari, yeye anasema kuwa "Mpaka leo Zanzibar hakuna gazeti binafsi. Kabla ya Mapinduzi kulikuwa na magazeti mengi, lakini historia ya uandishi wa habari Zanzibar imekufa kutokana na sheria zisizo rafiki."

Said Suleiman Ali, mchambuzi wa sheria, anaangazia Sheria ya Tume ya Utangazaji Na. 7 ya 1997, ambayo ilifanyiwa marekebisho mwaka 2010. Ananukuu:

“Kifungu cha 27(2) kinasema: 'Waziri anaweza kusitisha au kuzuia utangazaji wa redio au televisheni yoyote kwa sababu anazoziona kuwa ni kwa maslahi ya umma.”

Anaonya kuwa kifungu hicho kinampa waziri mamlaka ya juu kupita kiasi, hali inayodhoofisha uhuru wa vyombo vya habari.

Berema Suleiman Nassor, Mwandishi wa habari kutoka Zenj Fm Radio, anasema kuwa vyombo vya habari vingi haviandiki habari za  kukosoa hasa za kiuchunguzi kwa hofu ya kufungiwa.

"Hadhira inahitaji habari zenye kusisimua lakini tuna hofu ya kuandika habari hizo kwani ukiandika zinazogusa maslahi ya watu wenye mamlaka, biashara ya habari inakufa hapo hapo." Anasema

Katiba ya Zanzibar ya 1984, Kifungu cha 18 kinaeleza bayana kuwa uhuru wa kutoa maoni, kutafuta, kupokea  na kusambaza habari ni haki ya kola mtu.

"Kila mtu anayo haki na uhuru wa kutoa maoni, kutafuta, kupokea na kusambaza habari na mawazo yake kupitia chombo chochote cha habari bila ya kujali mipaka ya nchi." Kinafafanua kifungu hicho

Azimio la Kimataifa la Haki za Binadamu (UDHR), Ibara ya 19: inaeleza "Kila mtu ana haki ya kuwa na maoni na uhuru wa kujieleza; haki hii inajumuisha uhuru wa kushikilia maoni bila kuingiliwa, kutafuta, kupokea na kusambaza habari na mawazo kwa njia yoyote ile bila kujali mipaka."

Kwa upande wa Mkataba wa Afrika wa Haki za Binadamu na Watu (ACHPR), Ibara ya 9 nao unafafanua vyema kwa kusema "Kila mtu ana haki ya kupokea taarifa. Kila mtu ana haki ya kutoa maoni yake ndani ya sheria."

 

Post a Comment

0 Comments