Ticker

6/recent/ticker-posts

Mataifa Yanapiga Hatua, Sisi Tunaendelea Kukosa Sheria Rafiki

 


Na Ahmed Abdulla, Zanzibar

Katika zama hizi za teknolojia na habari zinazoenea kwa kasi, uhuru wa kujieleza ni msingi wa demokrasia, uwajibikaji wa viongozi na maendeleo ya kijamii. Haki hii ni dhamana inayotambuliwa kimataifa na inahitajika kulindwa na sheria rafiki kwa vyombo vya habari na wanahabari.

Lakini visiwani Zanzibar, hali ni tofauti. Kwa zaidi ya miongo mitatu, Sheria ya Wakala wa Habari, Magazeti na Vijarida Na. 5 ya 1988 bado ndiyo inasimamia sekta ya habari, huku wadau wakipaza sauti wakitaka mabadiliko yanayohakikisha uhuru wa kweli wa kujieleza.

Sheria hiyo inahitaji vyombo vya habari kupata ruhusa kabla ya kuanzishwa na inampa Waziri mamlaka ya kusimamisha au kupiga marufuku magazeti kwa maslahi ya taifa, mara nyingi bila utetezi wa mchapishaji.

Wakati Zanzibar ikiwa bado haijapata sharia inayotoa uhuru wa moja kwa moja kwa vyombo vya habari lakini yapo mataifa ambayo yana sharia bora za habari.

Miongoni mwa mataifa hayo kwa upande wa Afrika ni pamoja na Afrika Kusini ambayo Sheria yao ya habari Promotion of Access to Information Act (Sheria ya Kukuza Upatikanaji wa Taarifa) ya mwaka 2000 inaruhusu raia kupata taarifa kwa urahisi kutoka kwa taasisi za umma, ikichochea uwajibikaji wa serikali.

Nchi ya Ghana imejipambanuwa kwenye sharia bora ya habari Sheria ya Right to Information Act (Sheria ya Haki ya Kupata Habari) ya 2019 imeimarisha haki ya raia na wanahabari kupata habari bila vikwazo.

Afrika Mashariki ipo nchi ya Kenya ambayo Katiba yake ya mwaka 2010 inatambua uhuru wa vyombo vya habari na haki ya kupata taarifa kama haki za msingi za binadamu.

Lakini mbali na katiba lakini sheria zake za habari zinatoa uhuru wa moja kwa moja wa habari ikiwa ni pamoja na Sheria ya Upatikanaji wa Habari ya mwaka 2016.

Kifungu cha 5(1) kinaeleza kuwa “Kwa mujibu wa kifungu cha 6, shirika la umma litalazimika”

(a)            kuwezesha upatikanaji wa taarifa zinazoshikiliwa na chombo hicho na taarifa ambazo zinaweza kujumuisha.

Mbali na kuwepo kwa nchi hizo zenye sharia bora kwa Bara la Afrika lakini pia baadhi ya viongozi mbalimbali duniani wamenukuliwa wakisema maneno yaliyojaa dhamira ya kutaka uhuru wa habari katika ulimwengu.

Barack Obama Rais wa zanani wa Marekani alinukuliwa akisema kuwa “Vyombo vya habari huru si tishio kwa serikali nzuri; ni daraja la uwajibikaji.”

Kwa upande wa Justin Trudeau  Waziri Mkuu wa Canada yeye alinukuliwa akisema “Serikali inapaswa kuogopa kukosa ukosoaji, si kukosolewa.”

Kofi Annan Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa wa zamani yeye alisema kuwa “Uhuru wa vyombo vya habari ni msingi wa amani na maendeleo ya kijamii.”

Nelson Mandela Rais wa zamani wa Afrika Kusini  naye alisema “Sio tu tunahitaji uhuru wa siasa bali pia uhuru wa kusema ukweli.”

Angela Merkel Kansela wa zamani wa Ujerumani alisema “Demokrasia haiwezi kustawi bila vyombo vya habari huru na huru.”

 

Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, kupitia Kifungu cha 18, inatambua haki ya kila mtu ya kupata na kusambaza taarifa bila kuingiliwa.

Pia Zanzibar ni sehemu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo imeridhia mikataba muhimu ya haki za binadamu ikiwemo Mkataba wa Afrika wa Haki za Binadamu na Watu (ACHPR) na Mapendekezo ya UNESCO kuhusu Upatikanaji wa Habari lakini hata hivyo, sheria ya 1988 haijaendana na misingi hii.

Salma Said, mwandishi wa habari za maendeleo na mkurugenzi wa jumuiya ya waandishi wa habari za maendeleo Zanzibar (WAHAMAZA), alisema kuwa mazingira ya uandishi wa habari visiwani Zanzibar bado hayatoi uhuru wa kweli kwa wanahabari.

“Nimeshuhudia mara kadhaa waandishi wakijikuta mikononi mwa polisi, wakitishwa au hata vyombo vyao kufungiwa, hasa wanapoandika habari zinazogusa mamlaka au viongozi wa juu,” alisema Salma.

Aidha aliongezea kuwa hali hiyo imewafanya baadhi ya waandishi kuishi kwa hofu, na badala ya kuisemea jamii kwa uhuru, wanajikuta wakifanya kazi kwa kusita au kwa kumfurahisha mtu mmoja.

“Changamoto hizi zinatokana na vitisho vinavyozidi kushamiri, huku kukiwa hakuna sheria madhubuti ya kuwalinda wanahabari licha ya uwepo wa mikataba na matamko ya kimataifa yanayotambua haki zao,” aliongeza Salma.

Kwa upande wa Khairat Haji, kutoka Chama Cha Waandishi wa Habari Wanawake Zanzibar, TAMWA-Zanzibar, alieleza kuwa sheria zilizopo za habari visiwani Zanzibar zimekuwa kikwazo kwa uhuru wa uandishi, na kuwaweka waandishi katika mazingira magumu ya utendaji.

 “Waandishi wanapaswa kuendelea kupaza sauti juu ya ucheleweshaji wa mabadiliko ya sheria, na kusukuma mchakato wa marekebisho ufanyike kwa wakati.” Alieleza

Aidha, alitambua mchango wa vyombo vya habari vya kijamii katika kuelimisha wananchi kuhusu umuhimu wa sheria bora za habari:

“Redio za jamii zinafanya kazi kubwa ya kutoa uelewa kuhusu sheria za habari, jambo linalosaidia hata jamii za vijijini kufahamu haki zao na kushiriki katika mjadala wa kitaifa.” Aliongeza

Ripoti ya Baraza la Habari Tanzania (MCT) Zanzibar ya mwaka 2022/2023 inaweka wazi hali ngumu inayowakabili wanahabari katika kutekeleza majukumu yao visiwani. Ripoti hiyo inaeleza kuwa:

“Ofisi ya MCT Zanzibar ilirekodi jumla ya matukio 25 ya vitisho na vitendo vya unyanyasaji dhidi ya waandishi wa habari kwa mwaka wa 2017/2018. Matukio haya yalihusisha kunyimwa taarifa, unyanyasaji wa kimwili, waandishi kuzuiwa kuripoti baadhi ya matukio kwa sababu za kisiasa, na kunyimwa kadi za utambulisho.”

Ingawa ripoti hiyo ilichapishwa miaka ya nyuma, bado inaonyesha mifumo na changamoto zinazodumu, hasa kutokana na kutokuwepo kwa sheria rafiki ya habari inayolinda uhuru wa vyombo vya habari na wanahabari wenyewe.

 

Post a Comment

0 Comments