Ticker

6/recent/ticker-posts

Huduma ya kupima HIV yarejea Zanzibar, Vijana wamiminika Vituoni

 


Nafda Hindi, Zanzibar:

Vifaa vya kupimia maambukizi ya virusi vya ukimwi (HIV KITS) vyarejea Zanzibar baada ya kukosekana kwa takriban miezi mitatu katika Vituo vya Afya vya Serikali.

Hayo yamebainika baada ya Chama cha Waandishi wa habari  Wanawake TAMWA ZNZ kufanya ziara ya kutembelea Vituo vya Afya vilivyopo Wilaya ya Kati na Magharibi “B” Unguja na kugundua tatizo hilo kwa sasa limeshatatuliwa.

TAMWA ZNZ pamoja na waandishi wahabari walifika katika kituo cha Afya Mwera na kujionea hali halisi ya uwepo wa vifaa hivyo jambo linalotowa hamasa kwa vijana kurudi katika vituo hivyo  na kupima Afya zao bila ya usumbufu wowote.

Akizungumza na waandishi wahabari Afisa Ustawi wa jamii na mtoa huduma rafiki kwa vijana Kituo cha Afya Mwera Fatma Yussuf amesema baada ya kurudi kwa vifaa vifaa hivyo vijana wamehamasika kujitokeza kwa wingi kwa lengo la kupima Afya zao.

Amesema katika kituo hicho kwa siku wanapokea vijana wanane ambao wanafika kupima Afya zao hali ambayo inatowa matumaini kwa vijana kuishi kwa Amani kutokana na uwepo wa maradhi ya kuambukiza  ambayo husababisha kupoteza nguvu kazi ya Taifa hususan vijana.

“Vifaa tulivyoletewa vinaweza kutusogeza miezi mitatu, ila tunaomba tupatiwe vyengine kabla ya kumalizika vilivyopo ili tatizo hilo lisijitokeze tena,” Fatma Yussuf, alisema.

Nae Muelimishaji rika kwa vijana Kituo cha Afya Mwera Mwajuma Khatib  amesema kurejea kwa vifaa hivyo kunachangia ongezeko la vijana kujitokeza kwa wingi katika kituo hicho wakiamini ni mahali sahihi na kufurahishwa na utunzaji siri wa kituo kwa vijana ambao wamefika.

“Vijana wameelimika toka tupokee hizi kits wanaambiana kwamba mambo yetu tayari na wanajitokeza kwa wingi kwa sababu wanasema wana Amani na siri pia wako huru kwa lolote wanalouliza ukilinganisha na vituo vyengine vya binafsi,” Mwajuma Khatib alisema.

Nao vijana waliofika katika kituo hicho wamesema wanafurahia kurudi kwa huduma hiyo na watatumia fursa ya kupima Afya zao ili kujikinga na maradhi mbali mbali.

“ Mimi nina miaka 21, bado ni kijana nataka kuoa ndio maana napima Afya yangu mara kwa mara kuhakikisha niko salama , mimi situmii kinga kwa sababu ukitumia kinga haina ladha mwenzangu yeye hataki kutumia kinga ,” alisema Mohammed mkaazi wa Mwera.

Afisa Mradi wa Afya ya Uzazi kwa wasichana na wanawake  Zaina Abdalla Mzee amesema wamefarajika kuona vifaa vya kupimia virusi vya ukimwi kurejea katika vituo vya Afya vya Serikali baada ya ziara iliofanywa na TAMWA ZNZ na kugundua kuadimika kwa vifaa hivyo na waandishi wahabari kutekeleza jukumu lao la  kuandika habari  juu ya suala hilo.

“Kama tunavyojuwa kuwepo kwa vifaa hivyo ni muhimu kwa vijana na wananchi kwa jumla, hivyo tunaiomba Serikali kuwa na utaratibu maalum na wa uhakika kwa vifaa hivyo kwa sababu kukosekana kwake kunawasababisha vijana kukosa nafasi muhimu  ya kupima afya zao.

Mradi wa kuendeleza utetezi wa haki ya elimu ya Afya ya uzazi kwa vyombo vya habari kwa wasichana na wanawake  unaotekelezwa na TAMWA ZNZ ulitowa mafunzo kwa waandishi wa habari 71 na wahariri 23 kwa Unguja na Pemba ambapo ulioanza Octobet 2022 na kumalizika October 2023 ulitekelezwa kwa Wilaya ya Magharibi "B" na Kati kwa Unguja na Wilaya ya Chake Chake kwa Pemba.

 

 

 

 

        

Post a Comment

0 Comments