Ticker

6/recent/ticker-posts

Dkt. Mwinyi Azihimiza SMZ NA SMT Kushirikiana Kukuza Uchumi

 


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dk. Hussein Ali Mwinyi amehimiza ushirikiano wa kiutendaji baina ya taasisi za Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania (SMT) na za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) ili kuendeleza mageuzi ya uchumi na uwekezaji.

Dk. Mwinyi aliyasema hayo Ikulu, Zanzibar alipozungumza na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Mkumbo na ujumbe wake wa watu 20 waliofika kujitambulisha.

Alisema, SMZ na SMT wana ushirikiano mkubwa kwenye utendaji wa taasisi zao na kueleza, mara kadhaa taasisi ya hazina ya Zanzibar imekua ikipata ushirikiano mzuri na ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania pia Mamlaka ya Uwekezaji Zanzibar, ZIPA na TIC pamoja na taasisi nyengine za pande mbili hizo za Muungano hushirikiana katika kuboresha maendeleo kwa ustawi wa uchumi wa taifa la Tanzania na watu wake.

Rais Dk. Mwinyi pia alitumia fursa hiyo, kuwapongeza na kuushukuru ujumbe huo kwa utayari wao kwa kuendelea kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa mawazo ya mageuzi yanayolenga kujenga uchumi wa wananchi wa pande zote mbili za Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia ushirikiano uliopo baina ya tasisi za serikali mbili hizo, zikiwemo Mamlaka ya Bandari, Ofisi ya Msajili Hazina, Mamlaka za Uwekezaji pamoja na Tume ya Mipango ya Taifa.

“Niwapongeze kwa mawazo haya ya mageuzi, ni vizuri mara zote tuwe kunafikiria kujenga uchumi wetu kupitia taasisi zetu” alipongeza Rais Dk. Mwinyi.

Akiizungumzia bandari Jumuishi ya Mangapwaji Rais Dk. Mwinyi, alimueleza Waziri huyo kwamba SMZ imepania kuleta mageuzi makubwa ya uchumi kupitia bandari hiyo, ambayo kutokana na maumbile ya kisiwa cha Zanzibar kilivyo, inakusudiwa kujumuisha shughuli zote za badari mbali na kupakia na kushushia abiria na mizigo lakini kuruhusu meli mbalimbali za kimataifa zitakazoleta mageuzi makubwa ya biashara, uwekezaji na kuimarisha uchumi wa buluu.

Naye, Waziri Mkumbo alimuahidi Rais Dk. Mwinyi ushirikiano wa hali ya juu katika kuujenga uchumi wa nchi hasa kuelekea maadhimisho ya miaka 60 ya Muungano wa Tanzania na ya Mapinduzi ya Zanzibar wamejipanga kuleta mabadiliko makubwa ya uchumi.

Alisema, mbali na mambo mengine lakini kupitia mradi wa Bagamoyo, ujio wa Zanzibar umewaletea tija na ufanisi mkubwa kwenye utendaji wao hasa kwa taasisi wanazoshirikiana nazo kiutendaji kwani watajifunza mengi kupitia bandari jumishi ya Mangapwani pamoja na taasisi nyengine wanazoshirikiana nazo kiutendaji.

Ujumbe ulioongozana na Waziri Prof. Kitila umemjumuisha Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji  Dk. Tausi Kida, Msajili wa Hazina Bara, Nehemia Mchechu, Katibu wa Tume ya Mipango Lawrence Mafuru, Mkurugenzi Mkuu EPZA Charles Itembe, Mkurugenzi Mkuu TIC Gilead Teri na Mkurugenzi wa Miundombinu TPA Dk. Hussein Lufunyo.

IDARA YA MAWASILIANO IKULU, ZANZIBAR

Post a Comment

0 Comments