Ticker

6/recent/ticker-posts

Sheria Bora Ya Habari Itakua Demokrasia Z’bar


 

Na Ahmed Abdulla

 

DEMOKRASIA ni neno lenye uwanja mapana, lakini ikitekelezwa katika jamii ama katika nchi huwa kuna faida kubwa hasa ikizingatiwa kuwa hoja za wengi ndizo zinazofuatwa na kutekelezwa.

 

Hata hivyo, kwenye jamii yenye kuzingatia demokrasia ya kweli wachache kwa uchache wao nao husikilizwa hoja zaa na sio kupuuzwa na inapotokea hoja za wachache zina mantiki sio dhambi kutekelezwa.

 

Wataalamu wengi wanakubaliana kuwa uwepo wa vyombo vya habari vya aina mbalimbali una mchango mkubwa kwenye ujenzi wa demokrasia na pia suala la kupata habari linahesabiwa kama miongoni mwa haki muhimu za binaadamu.

 

Ili vyombo vya habari vitekeleze vyema jukumu la kujenga demokrasia katika nchi, lazima viwe huru katika kutekeleza majukumu yake pasiwepo na taasisi ama mtu ambaye kwa nguvu zake ama utashi wake atakuwa anaamrisha habari ipi itoke na ipi isitoke, pengine tu kwa maslahi yake sio maslahi ya jamii.

 

Uhuru huo wa vyombo vya habari katika nchi, lazima uambatane na uwepo wa sera, sheria na kanuni rafiki za habari zinazowawezesha wanahabari kutekeleza majukumu yao na sio kuwabana na lakini pasi na waandishi hao kuvunja sheria nyengine.

 

Kwa muda mrefu Zanzibar imekuwa na kilio cha kuwa na sheria mbovu za habari, ambapo msingi wa ubovu wa sheria hizo unatokana na kuwa ni za muda mrefu, kwa maana ya kwamba zimezeeka, zimechoka na kuchakaa.

 

Tunaposema sheria hizi zimekongweka maana yetu ni kwamba zimeshindwa kabisa kwenda na wakati, hasa kutokana na mabadiliko yanayotokea mara kwa mara kwenye tasnia ya habari yanayotokana na kukua kwa teknolojia.

 

Sheria nyingi za habari zilizopo Zanzibar ikiwemo ya magazeti na zinawapa nguvu viongozi ambazo hawastahiki kuwa nazo katika ulimwengu wa sasa wa demokrasia.

 

Kwa mfano sheria ya magazeti ya mwaka 1988, kifungu cha 30 (i) kinasema; “Endapo waziri anaona kuwa ni kwa manufaa ya umma au kwa maslahi ya amani na utulivu, anaweza kuamuru kufungiwa kwa gazeti... na gazeti hilo litakoma kuchapishwa kuanzia tarehe iliyotajwa.

 

Kwanini pasiwepo na bodi huru itakayoundwa na wataalamu kutoka serikalini, taasisi na mashirika binafsi ya habari yakachambua kuwa gazeti hilo limefanya kosa kadhaa na dhabu yake kadhaa.

 

Msingi wa kusema hivyo ni kwamba uwaziri ni wadhifa wa kisiasa kwa maana ya kwamba wakati mwengine anaweza asiwe mtaalamu wa habari lakini kapewa nafasi hii atakuwa na uwezo kiasi gani kitaalamu kubaini kosa la gazeti?

 

Mfano mwengine kifungu cha 48 cha sheria ya magazeti, kinaeleza makosa ikiwa ni pamoja na uchochezi na kashfa kwa mtu yeyote ambaye anachapisha, kuchapisha, kuuza, kusambaza au kutoa chapisho lolote la uchochezi na baada ya kukutwa na hatia mtu huyo faini au kifungo au vyote viwili faini na kifungo vitatolewa na uchapishaji huo utatolewa.

 

Hichi ni miongoni mwa kifungu ambacho sio tu kinapunguza uhuru wa vyombo vya habari, lakini pia kinahatarisha uhuru wa kujieleza kwa jumla, vifungu kama hivi vipo kwenye katiba na baadhi ya sheria za habari.

 

Serikali ya awamu ya nane imejipambanua kwenye ukuzaji demokrasia ndio maana iko tayari kuzirekebisha sheria zote zenye utata, hivyo sheria za bahari nazo umefika wakati kupitiwa tena upya.

 

Wadau wa habari wameshajadili sana na mapendezo yapo, serikali ione umuhimu wa kurekebisha sheria ili vyombo vyetu vya habari vikuze demokrasia nchini


Post a Comment

0 Comments