Shirika la Norwegian Church Aid - NCA limezindua rasmi Klabu ya Amani
ya Bodaboda -Tumbe Bodaboda Peace Club, inayowaleta pamoja vijana waendesha
bodaboda wa kijiji cha Tumbe, Wilaya ya Micheweni, Mkoa wa Kaskazini Pemba, kwa
lengo la kuwa mabalozi wa amani, mshikamano na majadiliano ya kujenga jamii
salama. Klabu hiyo ina wanachama 25, wote wakiwa vijana wa bodaboda ambao ni
sehemu muhimu ya jamii ya Tumbe na wanaochangia kwa kiasi kikubwa katika
shughuli za kijamii na kiuchumi.
Uzinduzi huo umefanyika katika ukumbi wa soko la wajasiriamali uliopo
Tumbe Mabatini n ani sehemu ya utekelezaji wa mradi wa Swahili Coast,
unaofadhiliwa na Royal Norwegian Embassy na kutekelezwa na NCA, ukilenga
kuhamasisha ushirikiano wa kiimani, uwezeshaji wa vijana na wanawake, pamoja na
kuzuia misimamo mikali katika ukanda wa pwani ya Tanzania.
Akizungumza katika hafla hiyo ya uzinduzi, Doreen Bwogi, Mratibu wa
Mradi wa Swahili Coast kutoka shirika la NCA Pemba, alieleza kuwa, kuanzishwa
kwa klabu hii ni hatua muhimu katika kuwakabidhi vijana nafasi ya kuwa walinzi
wa amani ya jamii yao. “Waendesha bodaboda mara nyingi wamekuwa wakionekana
kama chanzo cha migogoro, lakini kwa mtazamo wetu wao ni sehemu ya suluhisho.
Klabu hii imeanzishwa kwa lengo la kuwajengea uwezo wa kuwa viongozi wa
mabadiliko chanya,” alisema Doreen
Doreen alieleza kuwa NCA itaendelea kushirikiana na vijana hao katika
kuhakikisha wanakuwa na uelewa wa kutosha juu ya masuala ya amani, uraia,
usalama wa jamii na mapambano dhidi ya misimamo mikali. “Tumbe Bodaboda Peace
Club siyo tu klabu, ni harakati ya kuimarisha ustawi wa kijamii kwa kutumia
vijana kama daraja la mabadiliko,” aliongeza.
Katika hatua nyingine ya tukio hilo, Khelef Nassor, Afisa Utekelezaji Mradi
Msaidizi kutoka NCA, alitoa mafunzo kwa wanachama wote wa klabu, na kuwapa mwongozo
wa namna ya kuendesha klabu hiyo kwa ufanisi. Alisisitiza umuhimu wa kuwa na
vikao vya mara kwa mara, kuwa na uongozi shirikishi, na kushirikiana na taasisi
za serikali, dini na usalama katika kulinda amani ya kijiji.
“Klabu hii inapaswa kuwa mfano wa namna ambavyo vijana wanaweza kuwa
mstari wa mbele katika kusimamia masuala ya amani. Mnapaswa kuwa macho ya jamii
yenu, mtambue viashiria vya migogoro mapema, mkatae kuingizwa kwenye ajenda za
vurugu, na kuwa sehemu ya usuluhishi,” alisema Khelef wakati akizungumza
na wanachama wa klabu.
Mafunzo hayo yalihusisha pia mijadala ya wazi kuhusu uongozi chanya,
wajibu wa raia, usalama wa kijamii, na namna ya kushughulikia changamoto za
vijana wa bodaboda kwa njia ya mazungumzo na siyo kwa mabavu.
Wanachama wa klabu walipata nafasi ya kutoa maoni yao na kuelezea namna
wanavyoiona klabu hiyo kama fursa ya mabadiliko. Ali Matar, mmoja wa wanachama
wa klabu, alisema: “Tulizoea kuitwa wahuni, tukatengwa kwenye vikao vya
kijamii. Leo tuna klabu yetu, tunapewa nafasi ya kushiriki kwenye maamuzi na
kuelimika kuhusu amani. Hii ni hatua kubwa kwetu.”
Kwa upande wake, Mohammed Kombo, dereva wa bodaboda, alisema kuwa klabu
hiyo imekuja wakati muafaka ambapo vijana wengi wanahitaji miongozo ya kuacha
vishawishi vya vurugu na kujielekeza katika maendeleo. “Klabu hii imenipa
nguvu. Sasa najua siyo lazima kuwa mkali au mkimya ili usikike, unaweza
kusikilizwa kwa sababu ya mchango wako kwa jamii,” alisema.
Wanachama walitumia fursa hiyo kutoa shukrani kwa shirika la Norwegian Church
Aid - NCA na wafadhili wa mradi kwa kutambua nafasi ya vijana wa bodaboda
katika kuleta amani. Waliahidi kushirikiana kwa karibu na uongozi wa kijiji,
shehia, na viongozi wa dini katika kuimarisha usalama na mshikamano.
Akitoa salamu za uongozi wa shehia, Naibu Sheh awa shehia ya Tumbe Mashariki Bwana Makame Hassan Makame, alitoa pongezi kwa NCA na vijana wa bodaboda kwa kuanzisha klabu hiyo ya kipekee. Alieleza kuwa ni mara ya kwanza katika shehia yake kuona kundi la vijana wa bodaboda wakikusanyika si kwa ajili ya kazi pekee, bali kwa ajili ya kuijenga jamii yao. “Vijana hawa wameamua kusimama upande wa amani. Kama uongozi wa shehia, tutaendelea kushirikiana nao bega kwa bega kuhakikisha klabu hii inakuwa dira kwa vijana wengine. Naamini kupitia klabu hii, Tumbe itakuwa mfano wa kuigwa katika Pemba nzima,” alisema Makame.
Uzinduzi huo wa klabu ya amani ya Bodaboda umefungua ukurasa mpya kwa
vijana wa Tumbe, ambapo sasa wana jukwaa rasmi la kushiriki katika maamuzi ya
kijamii, kushiriki mafunzo ya uongozi, na kuandaa kampeni mbalimbali zenye
kuhamasisha mshikamano, usalama barabarani na maendeleo.
Kwa maneno ya wanachama wenyewe, “Tumbe Bodaboda Peace Club” ni
zaidi ya klabu, ni harakati ya kizazi kipya cha vijana waliojitoa kulinda
amani, kuunganisha jamii, na kusimamia mabadiliko ya kweli.
0 Comments