Ticker

6/recent/ticker-posts

Wanawake Na Wasichana Watakiwa Kushiriki Michezo Bila Ya Kuathiri Tamaduni Za Nchi Yao.

 


Na Asia Mwalim, Zanzibar:

WANAWAKE na watoto wa kike wametakiwa kushiriki michezo mbali mbali bila ya kukiuka mila na tamaduni za Kizanzibari ili kufaidika na fursa za michezo ndani na nje ya nchi.

Mkurugenzi wa Chama Cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania TAMWA-ZNZ, Dk. Mzuri Issa Ali alitoa wito huo wakati akifungua mafunzo ya Jinsia na michezo kwa waandishi wa habari huko Tunguu wilaya ya Kati Unguja.

Alisema wakati umefika wanawake na watoto wa kike kutumia fursa za michezo kuonesha uwezo wao na kufanikiwa kwenye maendeleo ya kifedha kupitia michezo kulingana na utamaduni wao.

Aidha alisema bado mapungufu ni makubwa kwenye michezo kutokana na wanawake kuachwa nyuma sambamba na kutozungumzwa sana kwenye vyombo vya habari.

Dk. Mzuri alitaja miongoni mwa faida za michezo ni pamoja na kuimarisha afya ya akili, mwili na kuongeza kipato jambo ambalo wanawake wengi wanalikosa 

Awali Afisa Programu wa mradi wa kuinua masuala ya jinsia kwenye Michezo, Khairat Haji Ali, alisema wameamua kuandaa mafunzo ya siku tano kwa waandishi wa habari ili kushajihisha michezo kwa wanawake na watoto wa kike.

Aidha alisema, lengo la mradi huo ni kufikia dhana ya usawa wa kijinsia kwenye michezo ikiwemo nafasi za kuongoza timu za mipira, na michezo mengi ne kwa wanawake sambamba na kuoatikana ushiriki wao kikamilifu.

Akiwasilisha mada katika mafunzo hayo, Mwaandishi habari mkongwe Haura Shamte, alisema ni vyema jamii kubadilisha mifumo ya malezi ili watoto wa kike wapate muda wa kushiriki vyema michezo kama ilivyo watoto wa kiume.

Baadhi ya washiriki wa mafunzo hayo walisema baadhi ya changamoto zinazorudisha nyuma jitihada za wanawake na watoto wa kike kushindwa kushiriki michezo ni kupewa majina mabaya, kuhusishwa na tabia chafu.

Mradi wa kukuza masuala ya jinsia kwenye michezo unatekelezwa na Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA-ZNZ), Jumuiya ya Wanasheria Wanawake Zanzibar (ZAFELA) na Kituo cha  Majadiliano kwa Vijana (CYD) ambao umedhaminiwa na Shirika la Ushirikiano wa Kimataifa wa Ujerumani (GIZ).

Post a Comment

0 Comments