Ticker

6/recent/ticker-posts

Wanawake Vinara Utendaji Baraza La Mawaziri Serikali Ya Awamu Ya Nane Zanzibar

 

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi akimuapisha Mhe,Salha Mohamed Mwinjuma kuwa Naibu Waziri wa Wizara ya Ardhi,Maendeleo ya Makaazi .kabla ya uteuzi alikuwa mwakilishi wa Viti maalum Kundi la Vijana Kusini,Unguja,hafla iliyofanyika leo viwanja vya Ikulu Jijini Zanzibar.

Na Ahmed Abdulla, Zanzibar

Mwanamke ni mlezi na mwanamke ni kiongozi.


Hii imedhihirika sio katika familia na jamii tu bali hata ndani ya muhimili muhimu wa dola wa kutunga na kuzilinda sheria za nchi – Baraza la Wawakilishi.


Uweledi huu wa viongozi ambao siku hizi, tafauti na dhana potofu iliokuwepo zamani, umethibitishwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduizi, Dk. Hussein Mwinyi.


Alisema’’Najivunia utendaji wa viongozi  wanawake katika serikali yangu, wakiwemo  mawaziri, makatibu wakuu, manaibu makatibu wakuu, wakuu wa mikoa na wilaya, wakurugenzi wa taasisi na mashirika ya umma’’.


Aliwapongeza wanawake aliowateua kushika nyadhifa mbali mbali za uongozi kwa kazi nzuri wanayofanya ambayo alisema anaridhika nayo.


Imani ya Dk. Mwinyi kwa wanawake kuonyesha uongozi bora ndio iliopelekea  wanawake kuongoza wizara sita kati ya 18.


Vile vile wapo manaibu mawazi wanawake watatu kati ya saba.


Baraza hilo limefanyiwa mabadiliko mara mbili tokea lilipoundwa mara ya kwanza na Rais Mwinyi na katika mabadiliko hayo hakuna waziri mwanamke aliyewekwa pembeni.


Hapo awali Baraza lilikuwa na wizara 15 na kati ya hizo wizara nne ziliongozwa na Wanawake. Nazo ni za Habari, Vijana na Utamaduni ambayo iliongozwa na  Tabia Mwita Maulid, Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makaazi iliyoongozwa na Riziki Pembe Juma, Wizara ya Utalii na Mambo ya Kale inayoshikwa   Lela Mohammed Mussa na Rahma Kassim Ali aliteuliwa Waziri wa ujenzi.


Mabadiliko yaliyofanywa mara ya kwanza na Dkt. Mwinyi ilikuwa ni faraja kwa wadau wanaopigania usawa wa kijinsia kwenye demokrasia na uongozi kwani licha ya kwamba hakuna Waziri waziri mwanamke aliyewekwa pembeni.


Baadaye pakaongezeka mawaziri wawili wanawake ambao, Dk. Saada Mkuya Salum aliyeshika Wizaza ya Nchi, Offisi ya Rais Fedha na Mipango na Harous Said Suleiman aliyeteuliwa  Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais.


Lakini jee wadau kupigania usawa wa kijinsia kwenye nafasi za uongozi na demokrasia wanaupimaje utendaji wao kwenye wizara walizopewa?


Maryam Ame amnbye ni Ofisa wa Mradi wa Kuwawezesha wanawake kushika nafasi uongozi kutoka Chama cha waandishi wa habari wanawake (TAMWA-Zanzibar) alisema kilichofanyika ni ishara ya matumaini kwa wanawake wanaotaka kuingia kwenye uongozi.


“Wanawaona wenzao kuwa wanaweza na wanazidi kuaminiwa” alisema.


 Alieleza wakati umefika kwa wanawake kujitokeza kushika nafasi za uongozi na kitu muhimu ni kuwa na sifa za uongozi na sio maumbile ya mtu.


Aliihimiza jamii kuacha kumuangalia mtu kwa jinsia yake bali elimu, uwezo na juhudi zake katika kazi.


 “Inawezekana ikawa ana elimu ya kawaida, lakini anaweza kuwa na uwezo mzuri wa kuongoza na kuzijua mbinu sahihi za kutatua changamoto za watu wake, kufuatilia matatizo ya kijamii na kuyapatia ufumbuzi”, aliongeza


Wanamichezo nao walizungumzia kufurahishwa na mabadiliko yanayoonekana ya wanawake kupewa nafasi za uongozi.

 

Katibu Mkuu wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Zanzibar (ZFF), Hussein Ahmada Vuai, alisema wanawame wamekuwa  wanatekeleza majukumu yao ya uongozi kikamilifu, iwe ni ya wizara, taasisi ama Shirika.


Alisema hata wizara inayohusika na michezo inaongozwa na wanawake kwenye nafasi za juu, akimaanisha Waziri na Katibu Mkuu na kufurahishwa kwamba wanatekeleza vyema  majukumu yao.


“Sisi kama ZFF tumekuwa tukitoa nafasi kwa wanawake katika kamati mbalimbali na wengini ni watendaji wakuu kwenye kamati hizo na wanafanya vizuri”, aliongeza.


Wanasiasa nao wamempongeza Dkt. Mwinyi kwa kuwaamini mawaziri wanawake.


Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake  wa CCM (UWT) wa Wilaya ya Amani Kichama, Francisca Camilius Climent, alisema wanawake wa CCM wamefarijika kuona Rais Mwinyi anavyowaamini wanawake.


“Hii kwetu ni faraja na inatutia nguvu kuona wanawake sasa tunashiriki kwenye vyombo  vya maamuzi ‘’, alidokeza.


Alisema hatua hii itawaongezea hamasa wanawake kuwania nafasi za uongozi na wanaopewa dhamana kufanya kazi kwa bidii.


Aliwataka wanawake waliopewa dhamana zanyadhifa mbalimbali  kufanya kazi kama walivyotarajiwa ili taifa lipate maendeleo.


Mnamo tarehe 27 Januari, mwaka huu, Rais Mwinyi  alifanya mabadiliko ya baraza la mawaziri yaliyohusisha  kuwateua wanawake wawili kushika nafasi za Manaibu waziri.


Nao ni  Salha Mohamed Mwinjuma kuwa Naibu Waziri wa Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makaazi na  Zawadi Amour Nassor kuwa Naibu Waziri wa Wizara ya Maji,Nishati na Madini.


Zanlight Blog ilipomtaka Salha Mohammed Mwinjuma na kuzungumzia uteuzi wake alisema anaamini uteuzi wa wanawake zaidi kushika nafasi za uongozi unatokana na kuthibitika kwamba wanao uwezo na uweledi wa kuongoza.


Aliwataka wanawake wengine wajifunze kutoka kwa viongozi waliowatangulia na mfano mzuri ni wa Rais wa Jamhuri ya Muungano, Mama Samia Suluhu Hassan na wanawake wengine waliowahi kuwa mawaziri au kushika nyadhifa nyengine za juu za uongozi.


Bahati Chumu Haji ambaye ni Naibu Katibu Mkuu wa Baraza la Wanawake la Chadema alisema imani ya Rais Mwinyi kwa wanawake ni hatua muhimu ya maendeleo.


“Hii kwa upande wetu wanawake inatutia moyo na kutufanya tujione ni watu muhimu na kuwa na ujasiri wa kufanya mambo muhimu kwenye nchi yetu” alisema Bi Bahati


Aliwanasihi wale waliopewa dhamana ya kuongoza taasisi mbalimbali kufanya kazi kwa bidii ili kuwabadilisha mtazamo wale wanaodhani  mwanamke hawezi kuongoza.

 

Kwa kweli sura ya uongozi Zanzibar inabadilika na kutoa matumaini ya kupatikana taswira inayoonyesha nafasi za uongozi ni sawa kwa wanaume na wanawake, ijapokuwa bado uwiano sio mzuri sana.

 

Hata hivyo hataua iliyopatikana katika miaka mitatu ya utawala wa Rais Mwinyi inatoa ishara kwamba safari ya kuelekea usawa wa uongozi unaopigiwa kelele inakwenda vizuri.

 

Lililo muhimu ni kwa wale waliokuwa na mashaka juu ya uwezo wa mwanamke kuongoza kubadilika na kuukubali kweli kwamba mwanamke mbali ya kuwa mlezi mzuri pia ni kiongozi mzuri.

 


Post a Comment

0 Comments