Ticker

6/recent/ticker-posts

Dkt. Mzuri: Tuelekeze Nguvu Kuwalinda Wanawake Na Watoto Wasidhalilishwe

 


Na Ahmed Abdulla Othman

 

MKURUGENZI wa Chama cha Waandishi wa habari Tanzania (TAMWA) Zanzibar Dk Mzuri Issa amesema kuwa licha ya adhabu kubwa inayotolewa kwa washtakiwa wa kesi za udhalilishaji lakini anashangaa kuwa matukio ya udhalilishaji yanaongezeka Zanzibar.

 

Aliyasema hayo wakati akifungua mkutano wa wadau wa masuala ya udhalilishaji uliolenga kujadili changamoto, mafanikio na nini kifanyike kutokomeza vitendo vya udhalilishaji.

 

Alisema kuwa hukumu za kesi za udhalilishaji zinazotolewa na Mahakama  zinaridhisha ikilinganishwa na miaka ya nyuma.

 

Alieleza anashangaa kuona matukio ya udhalilishaji yanaongezeka licha ya kwamba adhabu kubwa zinatolewa kwa washtakiwa wa makosa hayo.

 

"Hukumu zinazotolewa kwa washtakiwa wa kesi za udhalilishaji zinaridhisha tunashuhudia hukumu zinatolewa miaka 30 hadi 80 lakini sijui kwa nini matukio yanaongezeka"alisema Dk Mzuri.

 

Alieleza kuwa matukio ya udhalilishaji ikiwemo ubakaji yamekuwa yakifanywa na watu wa karibu katika familia ikiwemo Baba kubaka watoto wake.

 

Dk Mzuri alisema lazima kuwe na mikakati mipya ya ulinzi mkubwa kwa wanawake na watoto ili kutofanyiwa vitendo vya udhalilishaji.

 

Akieleza changamoto katika kushughulikia kesi za udhalilishaji wakili wa serikali kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa mashtaka Hamad Kombo, alisema mashahidi bado ni kikwazo katika kutoa ushahidi mahakamani hasa kwa wahanga wenyewe wa kike wenye umri kati ya miaka 14 hadi 17 ambao wamefanyiwa kitendo cha ubakaji.

 

Alisema wahanga hao wa udhalilishaji huwa wanawalinda wadhalilishaji kwa kutoa ushahidi wa uongo mahakamani au kukataa kutoa ushahidi kwa sababu huwa ni wapenzi.

 

Naye Ispekta wa Polisi kitoka dawati la jinsia Mkoa wa Kaskazini Pemba Fakihi Yussuf alisema wanafanya kazi katika mazingira magumu sana kufanya upelelezi wa kesi za udhalilishaji.

 

"Mimi binafsi natoa fedha zangu mfukoni kuwafuata mashahidi wa kesi za udhalilishaji wakati ninapofanya upelelezi wa kesi hizi......Polisi tunafanya kazi katika mazingira magumu sana katika mapambano ya kesi za udhalilishaji"alisema.

 

Akieleza mafanikio katika mapambano ya kesi hizo alisema kesi zinafikishwa mahakamani kwa haraka na kesi 15 zimetolewa hukumu kwa mwaka jana kwa Mkoa wa Kaskazini Pemba.

 

Kesi 168 za udhalilishaji zimeripotiwa Polisi katika Mkoa wa Kaskazini Pemba na kesi 144 zimeripotiwa Mkoa wa Kusini Unguja ambapo asilimia 20 ya watuhumiwa wa kesi hizo wamekimbia na bado hawajapatikana.


Post a Comment

0 Comments