Ticker

6/recent/ticker-posts

"WAFANYA BIASHARA PEMBEZONI MWA BARABARA TOWENI MASHIRIKIANO KWA WAJENZI WAKATI WA MATENGENEZO" RC KITWANA

 

MKUU wa Mkoa Mjini Magharibi Mhe Idrissa Kitwana Mustafa amewataka wananchi na wafanya biashara pembezoni mwa barabara itokayo wa uwanja wa Ndege hadi Kilimani kutoa mashirikiano kwa wajenzi wakati wa matengenezo ya barabara hiyo yatakapoanza.

 

Wito huo ameutoa wakati alipofanya ziara yake pamoja na watendaji wa taasisi mbali mbali huko maeneo ya Kiembesamaki ili kupanga namana ya kuanza kufanya kazi hiyo.

 

Amesema matengenezo ya misingi ya maji mvua na sehemu za watembea kwa miguu pembezoni mwa barabara hiyo yataanza mapema wiki hii ikiwa ni utekelezaji wa agizo alilolitoa Rais wa Zanzibar Dkt Hussen Ali Mwinyi wakati alipofanya ziara yake ya kukagua miradi ya ZUSP wiki iliyopita na kuagiza ndani ya miezi mitatu kuona mabadiliko barabara itokayo uwanaja wa ndege hadi mnazi mmoja.

 

“Mhe Rais alipofanya ziara katika eneo hili alitoa maagizo na maelekezo ya kuona mabadiliko ya haraka katika barabara hii na madelekezo yaliyotolewa kwetu sisi ni kazi,hivyo nikiwa kiongozi wa Mkoa huu nitahakikisha kazi hii inafanyika kwa haraka na wakati’alisema Mkuu wa Mkoa.

 

Aidha mkuu wa Mkoa ameziagiza taasisi zote ikiwemo ZUSP,ZAWA,Mawasiliano,Mamlaka ya Viwanja vya ndege na Manispaa kuanza kazi hiyo mara moja na kuikamilisha ndani ya miezi miwili kwa kiwango kinachotakiwa ili kuweka manzari ya maeneo hayo vizuri.

 

Hata hivyo ameeleza kufarajika na namna wafanyabiashara na wananchi wa maeneo hayo walivyo kuwa tayari kuunga mkono juhudi na hatua za serikali za kufanya matengenezo katika barabara ya uwanaja wa ndege.

 

Katika hatua nyengine mkuu wa Mkoa amewataka wafanya biashara kuhakikisha maeneo ya nje ya maduka yao yanakuwa safi na wasiweke bidhaa ili kuacha nafasi hizo kutumika na wananchi wanaotembea kwa miguu.

 

Nae mkurugenzi wa Baraza la Manispaa Magharibi B Ali Abdalla Natepe amesema iwapo taasisi hizo zitaendelea kushirikiana kwa pamoja upo uwezekano mkubwa wa kufanya kazi hiyo kwa ufanisi mkubwa huku akiwasisistiza wananchi kuacha kuweka taka chini na badala yake kutumia vifaa maalumu vya kutilia taka.

 

Amesema manispaa yake imejipanga kugawa  vifaa maalumu vya kutilia taka katika maduka yote yaliopo mbele ya barabara kuu ndani ya manispaa hiyo.

 

Mapema mwakilishi wa mamlaka ya viwanja vya ndege na wizara ya mawasiliano wamesema wataanza kazi hiyo kwa panmoja ili kuona maeneo yote wananyoyatengeneza yanakuwa na muonekano mmoja na wenye kuvutia.


Post a Comment

0 Comments