Ticker

6/recent/ticker-posts

"SEKTA ZA WIZARA YA HABARI TANZANI ZICHANGIE KUKUZA PATO LA TAIFA" INNOCENT BASHUNGWA


 

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe.Innocent Bashungwa amesema Wizara hiyo ni msingi wa kulinda historia, mila na desturi za nchi pamoja na kuhakikisha sekta zake zinachangia katika kukuza pato la taifa, ambapo amesisitiza kuwa sekta ya Michezo ina wajibu wa kuhakikisha inafanya vizuri ndani na nje ya nchi hivyo amewataka wataalamu wa Sekta hizo kuongeza ubunifu katika kutekeleza majukumu yao.

 

Mhe.Bashungwa ameyasema hayo leo Desemba 10,2020 katika kikao na Menejimenti ambayo ilijumuisha Wakuu wa Idara, Vitengo na Taasisi  zilizo chini ya wizara hiyo ambapo amesema ni jukumu la kila Idara na Taasisi kuwa na mtazamo chanya na kubuni njia mbalimbali za kitaalamu zitakazosaidia kutatua changamoto zilizopo katika sekta zao lengo likiwa ni kukidhi maatarajio ya kuundwa kwa Wizara hiyo.

 

"Ni lazima tuangalie namna ya kuchangia katika pato la taifa, pamoja na kuboresha makusanyo ya Mirabaha, Sekta ya Michezo leteni suluhisho la changamoto ambazo nyinyi wataalamu mnaona zitasaidia kuboresha sekta hii" alisema Bashungwa.

 

Mhe.Bashungwa ameongeza kuwa mkakati wa Serikali ni kuhakikisha Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) linasikika nchi nzima, hivyo fedha ambazo zimetengwa kwa ajili ya kuimarisha usikivu zitumike ipasavyo, huku akisisitiza Chama cha Hakimiliki Tanzania (COSOTA) kuendelea kutatua kero za wadau wake ili wanufaike na kazi zao.

 

Naye Naibu Waziri wa wizara hiyo Mhe. Abdallah Ulega amewaagiza wajumbe hao wa menejiment ya Wizara na Wakuu wa Taasisi kuangalia Sera zote zilizopo kama zinaendana na wakati uliopo na zinakidhi matakwa ya wadau wao na nchi katika kuendeleza sekta hizo.

 

Mhe.Ulega amesisitiza viongozi hao kuwa katika kulinda na kuendeleza maadili ya Kitanzania, mila na desturi za jamii  ni vyema kuwatumia viongozi wa dini ambao wanahudumia jamii kiimani, kimaadili na kielimu, Huku akihimiza Sekta ya michezo kuwa ina wajibu wa kutumia michezo ya UMITASHUMTA na UMISETA kuibua vipaji  vitavyosaidia kuzalisha wanamichezo.

 

Post a Comment

0 Comments