Ticker

6/recent/ticker-posts

Ulinzi Wanahabari Na Vyombo Vya Habari

 


Na Thuwaiba Habibu,Zanzibar:

Licha ya kuwa wanahabari ni wahabarishaji wakubwa wa umma  lakini wanakabiliwa na vikwazo vingi katika utendaji kazi zao ambavyo vinahatarisha usalama wa maisha yao ikiwamo kuuawa, udhalilishaji, utekwaji na uporwaji wa vifaa vyao; yote hayo hutokea kwa sababu hawana sheria rafiki ambayo ingeliweza kutoa ulinzi dhidi yao.

Hii imebainika baada ya waandishi wa habari kuonesha vikwazo vinavyotokea baada ya wao kukosa ulinzi

Mwandishi wa habari wa Mihra Tv 0nline Haji Bakari anasema  wakati vyombo vya habari vinakosa ulinzi, kuna uwezekano mkubwa wa kupungua kwa ubora wa taarifa zinazotolewa. na wanahabari wanaweza kujiwekea mipaka katika kuripoti habari muhimu kutokana na hofu inayowakabili.

Pia anasema kupungua kwa uhuru wa vyombo vya habari na ulinzi wa waandishi wa habari kunababisha waandishi wengi kufuata matakwa ya watu na siyo maadili ya  uandishi wa habari. anaeleza Haji.

"Bila ya kuwa na sheria rafiki za habari utendaji kazi wa waandishi wa habari unakuwa mgumu"

Mwandishi wa ZBC Tv Jamila Thabit Kombo anasema lipo tatizo la kupotosha taarifa; waandishi wa habari wanaweza kutoa taarifa ambayo si sahihi au kwa kutokutoa taarifa kabisa kwani kufanya hivyo ndiyo wanaamini watakuwa wamenusuru maisha yao na usalama.

Anasema  wanahabari wanaweza kuwa wahanga wa unyanyasaji, kama vile kutekwa, kupigwa, kuharibiwa vitendea kazi vyao, kuteremshwa kutoka kwenye chombo cha usafiri na kuachwa mwituni; Kusema kweli bila ya kuwapo kwa sheria zinazowalinda wanahabari kunawafanya wawe katika hatari kubwa zaidi ya unyanyasaji.

"Kuna mifano mingi ya waandishi ambayo tayari wameshafanyiwa unyanyasaji na bado hauwezi kukoma kwa sababu hakuna sheria inayowalinda,” anasema Jamila.

Mwandishi wa habari na Mjumbe wa Kamati ya Wataalamu  wa Masuala ya Habari Zanzibar (ZAMECO)  Jabir  Idirisa anasema yeye ni miongoni mwa waandishi waliokumbana na mashtaka kwa kufunguliwa kesi ambayo aliishi nayo kwa muda wa miaka 6  kuanzia  Januari 2016 hadi Septemba 2021 akituhumiwa kufanya uchochezi kwa kutimiza wajibu wake wa kutoa taarifa ambayo ni haki ya wananchi.

"Ni muhimu kuwa na sheria rafiki ambayo inaondoa hali ya kudhibiti sana  vyombo vya habari na itakuwa imewapa uhuru waandishi wa kufanya kazi zao."

Mwandishi Zulfa Juma Silima anasema vyombo vya habari vina jukumu muhimu katika kudumisha demokrasia. Kukosekana kwa ulinzi kunaweza kuathiri uwezo wao wa kuchunguza na kutoa taarifa kuhusu ufisadi, ukiukwaji wa haki za binadamu na masuala mengine ya kijamii.

"kukosekana kwa ulinzi wa vyombo vya habari na wanahabari kunaweza kuchangia changamoto nyingi ambazo zinaweza kuathiri si tu wanahabari wenyewe bali pia jamii nzima inayotegemea taarifa sahihi na huru."

 Katibu wa Klabu ya Waandishi wa Habari  Zanzibar  (ZPC) Mwinyimvua Abdi Nzukwi anasema kukosekana kwa ulinzi wa waandishi ndani ya sheria ya  Usajili wa Wakala wa Magazeti na Vitabu, Na 5 ya mwaka 1997 iliyofanyiwa marekebisho na Sheria Na. 8 mwaka 2010; ni kikwazo cha kutamani sheria ambayo itakuwa ndio mtetezi wao kwasababu sheria hii imeingiwa Mamlaka yake na  sekta nyengine.

"kukosekana kwa ulinzi kwa waandishi wa habari kupelekea waandishi kutowezesha kutoa baadhi ya taarifa na kufanya hivyo ni kuminya uhuru wa kujieleza na kutoa maoni  ambayo ni haki wa kila mtu"

Mkurugenzi wa Chama cha Waandishi wa Habari Tanzania (TAMWA-ZNZ ) anasema ulinzi na heshima ya waandishi wa habari ipo ndogo kwa Zanzibar, kwa wakati huu tuliona nao kama huheshimiki na huna ulinzi huwezi kuwa na uhuru wa kuandika habari.

Dr. Mzuri anasema ipo haja ya kuwapo sheria mpya ambayo pia itawahakikishia ulinzi na usalama wanahabari wanapofanya kazi zao.

Post a Comment

0 Comments