Ticker

6/recent/ticker-posts

"Sheria Bora ya Habari ni Dhamana ya Uchaguzi Huru" ZAMECO

 


Na Ahmed Abdulla:

Kila ifikapo tarehe 3 Mei, dunia huadhimisha Siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari Duniani, siku muhimu ya kutafakari nafasi ya vyombo vya habari katika kuendeleza demokrasia, uwazi, na maendeleo ya jamii.

Kwa mwaka huu, maadhimisho haya yamebeba uzito wa kipekee visiwani Zanzibar, ambapo kaulimbiu imeelekezwa kwenye uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 2025 huku kauli mbiu hiyo ikisema "Sheria nzuri ya Habari ni chachu ya uchaguzi ulio huru na wa haki."

Katika kuadhimisha siku hiyo, Kamati ya Wataalamu wa Masuala ya Habari Zanzibar (ZAMECO)  ikihusisha Klabu ya Waandishi wa Habari Zanzibar (ZPC), Cahama Cha Waandishi wa Habari Tanzania upande wa Zanzibar TAMWA-Zanzibar, Baraza la Habari Tanzania (MCT), Jumuiya ya Waandishi wa Habari za Maendeleo Zanzibar (WAHAMAZA) pamoja na Jukwaa la Watetezi wa Haki za Binadamu wameungana na jamii ya kimataifa kuhimiza upatikanaji wa sheria mpya ya habari itakayolinda uhuru wa vyombo vya habari na waandishi wake.

Mambo Matatu Muhimu Yanayoainishwa na ZAMECO:


ZAMECO inasisitiza kuwa ipo haja ya haraka kupatikana kwa sheria mpya ya habari itakayozingatia Katiba, mikataba ya kikanda na kimataifa juu ya uhuru wa kujieleza, pamoja na maoni ya wadau.

Sheria hiyo itasaidia kujenga msingi wa uchaguzi ulio huru, wenye haki na uwazi” inaeleza taarifa hiyo

Aidha kamati hiyo inasema Katika kipindi cha uchaguzi, waandishi wa habari huwa mstari wa mbele kufikisha taarifa kwa umma. Hata hivyo, bado wapo katika hatari ya vitisho, mashambulizi na unyanyasaji.

Hivyo ZAMECO inatoa wito kwa vyombo vya dola, vyama vya siasa na wadau wengine kuhakikisha waandishi wanalindwa kikamilifu wanapotekeleza majukumu yao.


sambamba na hayo ZAMECO inakemea vikali ubaguzi wowote dhidi ya vyombo vya habari  iwe kwa misingi ya kiitikadi, aina ya chombo au mtazamo wa mhariri.

Pia wanatilia mkazo kuwa utaratibu wa utoaji wa kadi za kuripoti kutoka Tume ya Uchaguzi uwe wazi, shirikishi, na usiomwondoa mwandishi yeyote mwenye sifa.

Wito kwa Serikali na Wadau

Katika hitimisho la taarifa yao, ZAMECO inatoa wito kwa serikali ya Zanzibar na Tume ya Uchaguzi kuonyesha dhamira ya kweli kwa kuhakikisha waandishi wanapewa nafasi, heshima na ulinzi wanaostahili katika utekelezaji wa majukumu yao.

Aidha, waandishi wa habari na mashirika yao wanahimizwa kuendelea kudai haki zao kwa njia za amani, na kuwa mstari wa mbele kulinda misingi ya uwazi na uwajibikaji katika jamii.

"Kuwapo kwa Uhuru wa Habari ni chachu ya maendeleo katika nchi." Inamalizia taarifa ya ZAMECO

 

Post a Comment

0 Comments