Ticker

6/recent/ticker-posts

Dkt. Mwinyi Aipongeza Zawiyyatul Qadita Kwa Kumuombea Duwa Mzee Mwinyi


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Al hajj Dk. Hussein Ali Mwinyi ametoa shukurani zake za dhati kwa Jumuiya ya Zawiyyatul Qadiria - Tanzania iliyomuombea dua Hayati Mzee Ali Hassan Mwinyi.

Al hajj Dk. Mwinyi alitoa shukurani hizo baada ya Ibada ya sala ya Ijumaa iliyoambatana na dua maalum ya kumuombea Hayati Mzee Ali Hassan Mwinyi, Rais mstaafu wa Zanzibar na Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, huko Masjid Ngamia Welezo, Mkoa wa Mjini Magharibi.

Al hajj Rais Dk. Mwinyi alishukuru Jumuiya hiyo kwa niaba ya familia yake, pamoja na kuwataka waumini wa dini ya Kiislam kuendelea kumuombea dua Marehemu Mzee Mwinyi pamoja na kuliombea taifa ili liendelee kudumu kwenye amani na utulivu.

“Tuendelee kumuombea dua Mzee wetu, tuendelee kuiombea dua nchi yetu iendelee kudumu kwenye amani tuliyokuwa nayo na Mwenyezi Mungu atupe wepesi katika majukumu yetu” Alisisitiza Al hajj Dk. Mwinyi.

Marehemu Mzee Ali Hassan Mwenyi alifariki dunia Febuari 29 mwaka huu, Dar es Salaam na kuzikwa Machi 02, 2024 Mangapwani, Mkoa wa Kaskazini Unguja.

Akizungumza kwenye hafla ya dua hiyo, Kadhi Mkuu wa Zanzibar, Sheikh Hassan Othman Ngwali mbali na kumpa pole Al haj Dk. Mwinyi kwa msiba wa mzee wake uliotokea hivi karibuni lakini pia alitoa shukurani kwa waislam wote waliohudhuria ibada ya sala ya Ijumaa pamoja na dua maalum ya kumuombea Hayati Mzee Ali Hassan Mwinyi pamoja na kuiasa jamii kuongeza ushirikiano kwenye masuala ya kijamii.

Naye Khatib wa ibada ya Sala ya Ijumaa, msikitini hapo aliwataka waumini wa Kiislam kukithirisha sana ibada kipindi hiki cha Mwezi Mtukufu wa Ramadhan kwa kuendelea kusoma Quran tukufu, kutoa sadaka kwani huweka wepesi wa wamchao Mola, pamoja na kushajihisha jamii kusaidiana kwa kufutarishana hasa kwa wasiokuwa na uwezo kusaidiwa zaidi kipindi hiki.

Sambamba na kuueleza kwamba kila inapofika mwezi Mtukufu wa Ramadhan Mwenyezi Mungu (S.W) huifungua milano yote ya Pepo na kuifunga milango saba ya Moto pamoja na mashetani kufungwa ili kutoa fursa nzuri kwa waumini wa kiislam kufanya ibada kwa uhuru.

Akitoa historia ya fupi ya Jumuiya ya Zawiyyatul Qadiria – Tanzania, Mkurugenzi wa huduma nyenginezo wa Jumuiya hiyo, Sheikh Siasa, alisema iliasisiwa mwaka 1988 Tanzania Bara na baadae mwaka 1992 lilifunguliwa tawi lake Zanzibar likiongozwa na mlezi wake Sheikh Said Othman Abdul Kadir Othman bin Muhammed bin Nuur.

Post a Comment

0 Comments