Ticker

6/recent/ticker-posts

Malezi Ya Watoto Ni Wajibu Kwa Wazazi Wawili

 

Ummulkuthum Omar Daktari Bingwa wa magojwa ya kike na Uzazi kutoka Hospitali ya Mnazi Mmoja Zanzibar


Na Nihifadhi Abdulla Issa:

Dhana ya malezi katika jamii imezoeleka ni pale mtoto anapozaliwa ndipo hutayarishiwa mfumo wa malezi kwa baadhi ya familia kwa kupata huduma stahiki ikiwa ni pamoja na malezi na uangalizi wa wazee na jamii iliomzunguka.

Dhana hii inakwenda mbali zaidi kwa baadhi ya wanaume na jamii kuona kwamba ujauzito hauhitaji uangalizi na matunzo bali kile kinachozaliwa ndicho kinachostahiki maandalizi na matunzo .

Tukirudi nyuma kidogo kuangalia Msemo wa Wahenga husema  “Kulea mimba si kazi bali kulea mwana ndio kazi”.

Kwa dunia ya sasa msemo huu hauwendi na wakati uliopo kutokana na ugumu wa kazi nzito ya kulea mimba kwa mazingira ya wakati huu na kukabiliwa na vikwazo kadhaa ikiwemo maradhi na magonjwa tofauti ukilinganisha na zama walizoishi mababu na mabibi zetu.

Hatusemi kwamba kwa wakati huo hakukuwa na maradhi na magonjwa ingawa ni kwa kiasi kidogo mno ukilinganisha na wakati wa sasa wa sayansi na teknologia.

MTAALAM  WA AFYA

Wakati jamii ikiamini hivyo kwa upande wa malezi na huduma kwa mtoto wataalam wa Afya kwa upande wao wana mitazamo yao ya kitaalam inayoelezea dhana hiyo kwa upana.

Daktari Bingwa wa magojwa ya kike na Uzazi Dk Ummulkuthum Omar kutoka Hospitali ya Rufaa  Mnazi Mmoja amesema kwa upande wa Afya ya Uzazi kiujumla huanzia tokea pale mimba itapotunga kwenye fuko la uzazi hadi kuzaliwa na hapo ndipo yanapoanza malezi hasa.

Dk Ummulkulthum amesema suala la Afya ya Uzazi linaanzia mbali sio kama watu wanavyofikiria toka siku mtoto akizaliwa mpaka anakufa anaishi katika dhana ya Afya ya Uzazi.

“Suala la Afya ya Uzazi si la mwanamke tu bali ni la mtoto wa kike na wa kiume kwa sababu huwezi kuzaa bila ya mwanamme, hivyo hata katika malezi na makuzi ya mtoto ni lazima kushirikiana kwa pamoja kwa mustakabali wa ustawi wa mtoto kiakili na hata kimwili, Dkt Ummulkuthum Omar Daktari Bingwa magonjwa ya kike na Uzazi.

MUAMKO WA WAZAZI

Fatma Juma 27 mkaazi wa Kinuni Mkoa wa Mjini Magharib amesema mume wake hajapata Elimu ya Afya ya Uzazi hali inayopelekea kutokuwajibika ipasavyo katika majukumu ya pamoja ya kulea mimba na hata watoto.

“Mume wangu hana taalum ya Afya ya Uzazi yeye anachojuwa ni kutafuta kula ndio jukumu lake na akifanikiwa ndio hilo limeisha ila masuala ya kushiriki katika mambo ya nyumbani kama vile kunisaidia kazi za nyumbani anasema sio jukumu lake kwa sababu akitoka asubuhi kwenda kazini mpaka usiku.

Mohd Ali 43 mkaazi wa Maungani anasema mtoto ni lazima alilewe kwa mashirikiano ya wazazi wa pande zote ila inakuwa ni kikwazo kwa sababu majukumu kwa wananume yanakuwa ni mengi anatakiwa kutoka kwenda kutafuta mahitaji ya nyumbani.

“Mimi ni mzazi na nawajibika kulea sikatai lakini ni lazima kutoka asubuhi kwenda kazini kutafuta mahitaji na mke wangu ndio anabaki na watoto kwa ajili ya malezi na majukumu ya nyumbani,” alisema.

Baadhi ya wazazi wanawake walikuwa na mawazo tofauti kwamba kutokana na hali ya sasa imebadilika tofauti na zamani , kwa sababu wazee wote wawili wanatika kwenda kazini kutafuta maisha kutokana na ugumu wa maisha.

“Mimi ni mama wa watoto watatu lakini pia ni mfanyakazi, nalazimika kutoka asubuhi kuwahi kazini kutekeleza majukumu mengine na kuwaacha watoto wangu na mlezi, alisema mzazi.

Rukayya Aali Hassan mkaazi wa Kwahani  36 anasema  kutokana na hali ya maisha ya sasa imebadilika hivyo imesababisha watoto kukosa muda stahiki wa malezi kwa wazazi ama jamaa zao wa karibu kama ilivyokuwa hapo awali (zamani).

“Mzee wangu alikuwa anafanya kazi ni muajiriwa Serikalilini, ni Mwalimu wa Skuli sisi tumezaliwa tisa lakini tulilelewa na bibi yetu mzaa mama, wakati mama anakwenda kazini bibi yupo nyumbani analea wajukuun zake,” alisema Rukayya.

Bakar Faki 25, mkaazi wa Fuoni Unguja amesema wanaume wana jukumu la kutoka nje kwenda kutafuta matumizi ya mke na watoto kama vile chakula na mahitaji mengine ya lazima hivyo jukumu la malezi na mambo ya nyumbani ni wajibu wa mwanamke ambae umemuowa.

“ Nikitoka asubuhi mpaka asubuhi kwa hiyo changamoto za malezi kwa mchana wa kutwa zinamkuta mwanamke, nikirudi napewa kesi nasuluhisha ndo maisha tuanayoishi mimi na mke wangu,” alisema Bakar.

DINI YA KIISLAM INASEMAJE KUHUSU JUKUMU LA MALEZI SHEIKH KHAMIS ABDULHAMID

Malezi ya mtoto huanzia mbali tokea taratibum za kutafuta mchumba hadi kufikia ndoa yenyewe na utekelezaji wa majukumu yake ipasavyo.

Sheikh Khamis Abdulhamid kutoka Baraza la Maulamaa Zanzibar  akizungumzia mada juu ya malezi ya watoto katika Uislam alianzia mbali na kusema katika kitabu kitukufu cha QUR AN kimeeleza wazi kuhusu jambo hilo,

Sheikh Khamis alitaja Sura mbali mbali za QUR AN kama vile Suratul Nnisai na Hujrat zinazungumzia malezi ya watoto kwa kusema Mwanamme ni mlezi au msimamizi kwa mwanamke na si Kiongozi na majukumu ya nyumba ni ya mwanamme na asiesimamia ana dhambi na atalipwa.

“Baadhi ya wanaume wanatafsiri vibaya aya hii hata kama mwanamke anafanya kazi ni hisani yake tu kukupa bali si wajibu wake,” Sheikh Abduhamid .

Aidha Aalim huyo alisema Baba ndio mwenye jukumu la kulea watoto na akenda kinyume na wajibu aliopewa basi sheria za Allah za zitamkamata.

Akifafanua kuhusu ndoa amesema suala la Ndoa ni Sheria pia ni Sunna lakini hubadilika kuwa dhambi endapo hutoitendea haki akithibitisha maneno hayo kutoka katika kitabu kitakatifu QUR AN Suratul Annur, Aya ya 33.

“Wajizuie wale wanaume kutokuowa mpaka atakapowapa uwezo Mola wa,” Sheikh Khamis Abdulhamid.

Hata hivyo amesema Suratul Talaqa imetoa ufafanuzi mzuri kuhusu haki ya mwanamke na mtoto (yaani malezi ) wakati wa kumuacha mke kumpatia haki zake ikiwa ana mtoto  anaenyonyesha mtoto wako ni wajibu kumlipa (kumpa fidia).

“ Ikiwa ndani ya ndoa si lazima kumlipa bali mukiachana ikiwa atakunyonyeshea mwanao sheria ya dini ya Kiislam inasema umlipe,” Sheikh Khamis.

Sheikh Khamis Abdulhamid kutoka Baraza la Maulamaa Zanzibar


SKULI ZINAZOTUMIKA KWA UANGALIZI KWA MTOTO (BABY CARE)

Mkuu wa Taaluma wa Skuli ya Pasira ilioko Kianga, Mkoa wa Mjini Magharibi, Wilaya ya Magharibi ‘’A” Deleta Said Othman amesema skuli hizo wazazi wanapeleka watoto wao kutokana na kukosa muda muafaka wa kulea wakiwa wafanyakazi (wameajiriwa).

Othman amesema muamko wazazi kuwapeleka watoto katika skuli hizo hutegemea malezi na mtoto kufundishwa kujitegemea mwenyewe ukilinganisha na kumpeleka kwa mlezi wa kawaida hupata malezi tu bali na kufundishwa kujitegemea na kufanya baadhi ya mambo yake mwenyewe  kama vile baada ya kula kuondosha sahani yake mwenyewe.

“Kulea watoto wadogo ni kazi  lakini tunakumbana na changamoto mbali mbali kama vile kwenye mfumo mzima wa chakula mfano unampa uji analia lakini pia kuzoea mazingira watoto hulia sana, na wanahitaji uangalizi wa hali ya juu kwa  kwa sababu hupokea maradhi mara moja ukilinganisha na watoto wakubwa hiyo inabidi uache kazi kuwashughulikia,” Deleta Othman, Mkuu wa Taaluma Pasira.

Hata hivyo Othman amesma katika vituo hivyo wataalam wa Afya hupita mara mbili mpaka tatu kwa mwaka kuangalia Afya ikiwemo usafi wa vyoo na mazingira halisi ili kuwalinda watoto na athari zinazoweza kujitokeza kiafya.

MFANYAKAZI KATIKA SKULI YA PASIRA

Zulfa Khamis 30 ni mama wa watoto watatu mkaazi wa Mwera anasema kazi ya ulezi ni ngumu hasa ukizingatia watoto bado ni wadogo sana hawajaweza kujitambuwa na wengine hata kuzungumza hawajajuwa vizuri kwa hiyo inatuwia vigumu uache kazi ufanye kazi.

“Watoto ni wadogo sana kuanzia miaka miwili wana kazi sana, kazi ya ulezi si lele mama ujipange na ndio maana baadhi ya wazazi huwapeleka watoto wao kwenye vituo vya kulelea kwa sababu ulezi ni kazi nzito,” alisema Zulfa.

MTAALAM WA SAIKOLOJIA

Kutokana na tatizo la kulelewa watoto nje ya familia zao au vituo vya kulelea watoto huathiri akili ya mtoto mwenyewe na familia kwa ujumla na hata ukuwaji wake kwa sababu wanahitaji uangalizi wa hali ya juu.

Mtaalam wa Saikolojia Amina Khalfan kutoka Hospitali ya wagonjwa wa Akili Kidongo Chekundu Wilaya ya Mjini anasema watoto kuwa mbali na familia zao au watu waliowazoea huleta athari kwao kwa ukuwaji lakini hata kiakili.

“Watoto wanakabiliwa na upweke kwanza, lakini hata kubadilishwa mazingira mpaka kuyazoea inachukuwa mda na vile vile huga tabia za watu wengine wapya waliowazunguka na si za familia zao kama zamani tulivyolele sisi,” Alisema Amina, Mtaalam wa Saikolojia.

Chanzo cha watoto kutolelewa na wazazi au watu wao wa karibu kunachangiwa na sababu kadhaa zikiwemo za kiuchumi na hata mogogoro ya familia kama vile kuachana kwa baba na mama na mtoto kulelewa na mzazi mmoja hivyo ipo haja kwa jamii kukaa chini na kuangali akwa namna gani kulitafutia ufumbuzi ama muarubaini tatizo hili kwa kuokowa nguvu kazi ya Taifa.

Mradi wa Afya ya Uzazi Wasichana  na Wanawake umefadhiliwa na Shirika la Wellspring Philanthropic Fund la Marekani.

Kwa sasa mradi huu unatekelezwa na Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake kwa Upande wa Bara na Zanzibar kwa lengo la kuongeza ushawishi na utetezi kwa kupitia vyombo vya habari juu ya umuhimu wa upatikanaji wa huduma ya Afya ya Uzazi kwa wasichana na wanawake

Post a Comment

0 Comments